JESHI LA POLISI ARUSHA LATOA UFAFANUZI TUKIO LA WAANDISHI WA HABARI WA GLOBAL TV NA TRIPPLE A RADIO

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha ACP Justine Masejo

Na mwandishi wetu Arusha
Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha limetoa ufafanuzi kuhusu tukio la Waandishi wa habari wawili Korumba Victor Moshi wa Global Tv na Alphonce Kusaga wa Tripple A Radio.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha ACP Justine Masejo akiongea na vyombo vya habari leo February 26, amesema kuwa Tarehe 24.02.2022 muda wa saa 4:00 asubuhi huko maeneo ya Sakina katika Halmashuri ya Jiji la Arusha askari wa jeshi la akiba (mgambo) waliwakamata Ester Jackson (38) na Isaya Mollel (20) wote wakazi wa Ngaramtoni wakiwa na Bhangi misokoto 1755 na kuwafikisha katika kituo kidogo cha Polisi Sakina.

Kamanda Masejo ameendelea kusema kuwa baada ya tukio hilo, baadhi ya watu waliwasiliana na waandishi wa habari kuhusiana na tukio la kukamatwa kwa watuhumiwa hao ambapo walifika eneo la tukio na kuanza kufanya mahojiano na baadhi ya wananchi ambao walishuhudia tukio hilo.

Wakati waandishi hao wakiendelea kuwahoji watu katika eneo la Raskazoni, askari mgambo hao walipita katika eneo hilo ambapo inadaiwa waandishi hao waliwasimamisha kwa lengo la kuwahoji, kitendo hicho pamoja na kupigwa picha kiliibua mzozo kati ya waandishi hao na askari wa mgambo.

Amesema waliendelea kuvutana kuanzia eneo la Raskazoni hadi eneo la Sakina kilipo kituo cha Polisi na kusababisha vurugu eneo hilo.

ACP Masejo amewaambia waandishi kuwa askari polisi waliokuwa zamu katika kituo hicho waliomba msaada kutoka kituo cha Polisi kati (Central), kutokana na idadi ya watu kuanza kuongezeka katika kituo hicho, ndipo Mkuu wa kituo cha Polisi Kati alifika kituoni hapo na kuwachukua waandishi hao wa habari pamoja na mgambo kwa ajili ya mahojiano, ambapo waliachiwa baada ya kuhojiwa.

Kamanda Masejo amesema baada ya kupata maelezo ya watu mbalimbali walioshuhudia kuanzia chanzo cha mzozo huo, tutapeleka jalada kwa Mwendesha Mashtaka wa Serikali kwa maamuzi ya kisheria.

ACP Masejo amesema Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha litaendelea kuhakikisha wananchi wakiwepo waandishi wa habari wanaendelea kufanya shughuli zao katika mazingira ya amani, utulivu na usalama kwa kufuata sheria, kanuni na taratibu za nchi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments