MZEE NATABAY AFARIKI AKIWA NA UMRI WA MIAKA 127...FAMILIA YAOMBA AINGIE KWENYE KITABU CHA GUINNESS WORLD RECORDS


Mzee mmoja aitwaye Natabay Tinsiew huko nchini Eritrea amefariki akiwa na umri wa miaka 127, familia yake imesema.

Aidha familia hiyo imesema ina matumaini kwamba Natabay Tinsiew atapata nafasi ya kuandikwa kwenye kitabu cha Guinness World Records kama mtu aliyewahi kuishi miaka mingi zaidi.

"Uvumilivu, ukarimu na maisha ya furaha" ndio siri ya mzee huyo kuishi kwa muda mrefu, mjukuu wake Zere Natabay aliiambia BBC Tigrinya.

Bwana Natabay alifariki siku ya Jumatatu akiwa na amani katika kijiji chake, Azefa - ambacho kina idadi ya watu takribani 300 na kipo kwenye korongo lililozungukwa na milima.

Mjukuu wake amesema rekodi za kanisa - pamoja na cheti chake cha kuzaliwa - kinaonesha kuwa alizaliwa mnamo mwaka 1894 - na ndio mwaka ambao alibatizwa - na hivyo kumfanya awe amefariki akiwa na miaka 127.

Lakini familia ya Bw. Natabay inaamini kuwa mzee huyo alizaliwa mnamo mwaka 1884, lakini alibatizwa miaka 10 baadaye, wakati mapadre walipokuja karibu na kijijini kwao.Kulikuwa na mapadre wachache wakati huo, na watu walikuwa wakiwasubiri watembelee kijiji chao.

Padre Mentay, wa kanisa katoliki ambaye alihudumu katika kijiji hicho kwa miaka saba, alithibitisha kwamba rekodi zilionesha kwamba Bwana Natabay alizaliwa mnamo 1894. Alisema alikuwepo wakati wanakijiji wakisherehekea alipotimiza miaka 120 mnamo 2014.

Bwana Zere aliiambia BBC kuwa tayari alikuwa amewasiliana na Guinness World Record ili kuthibitisha hati rasmi za kuzaliwa kwa babu yake, na alikuwa akingojea kusikia kutoka kwao.

Katika kitabu cha Guinness World Records kimemrekodi mwanamke wa Ufaransa Jeanne Calment, aliyekufariki mnamo 1997 akiwa na miaka 122, kama mtu aliyeishi miaka mingi zaidi.

Bwana Natabay alioa mnamo mwaka 1934, mke wake alifariki mwaka 2019 akiwa na umri wa miaka 99.

Wakati wa maisha yake, Bwana Natabay alikuwa mfugaji, mwenye ng'ombe wengi, mbuzi na nyuki.

Vilevile alifanikiwa kuishi na kuona vizazi vitano vya familia yake vikikua.

Bwana Zere alisema babu yake atakumbukwa kama "mtu wa kushangaza", ambaye alikuwa mwema, anayejali na mchapa kazi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments