JAJI MKUU PROF JUMA AWATAKA MAJAJI KUZINGATIA MAADILI ,UADILIFU NA KUMTANGULIZA MUNGU MBELE


Jaji mkuu wa Tanzania Profesa Ibrahim Juma akifungua mafunzo hayo
Jaji mkuu wa Tanzania Profesa Ibrahim Juma amewataka majaji wa mahakama ya rufaa na mahakama kuu kutoogopa kusema au kutoa taarifa katika vyombo husika wanapobaini mapungufu katika sheria.

Jaji Mkuu Juma ametoa rai hiyo wakati akifungua mafunzo elekezi kwa majaji 31 wa mahakama ya rufaa na mahakama kuu Tanzania Bara na Visiwani ambao waliteuliwa na kuapishwa hivi karibuni na Rais Samia Suluhu Hassan yaliyofanyika katika Chuo Cha Uongozi wa mahakama (IJA) kilichopo Lushoto Tanga.

Jaji Mkuu Juma aliwataka majaji kuzingatia maadili na uadilifu na kumuweka Mungu mbele katika maamuzi yao kwa sababu maamuzi hayo yanagusa maisha ya watu wengi.

Akisisitiza juu ya jukumu la majaji kuwa watafsiri wakuu wa sheria, alisema kuwa wanapokwenda kufanya kazi watakutana na mapungufu ya sheria na kusema kuwa kazi kubwa ya majaji ni kutafsiri sheria na katiba.

Profesa Juma alisema kuwa majaji wajielewe kuwa wao ni viongozi na sehemu ya maboresho hivyo wasikae kimya wanapobaini mapungufu katika sheria ili zifanyiwe maboresho kwa faida ya watanzania.

Alisema kuwa katiba imewakopesha viongozi hao wa mahakama mambo Fulani na kubakisha mambo mengine ambayo ni haki za wananchi zinazotakiwa kulindwa.

Kwa upande wake Jaji Kiongozi Eliezer Feleshi alisema mafunzo hayo ni ya pili kufanyika kwa majaji wa rufaa, ya sita kwa majaji wa mahakama kuu, na mara ya pili kwa majaji wa Tanzania bara na visiwani.

Alisema mafunzo hayo ni uthibitisho kuwa maboresho yanajengewa misingi bora ya utekelezaji.

Pia jaji huyo kiongozi alikisifu Chuo cha Mahakama kwa kuwa msaada kwa kuandaa mafunzo hayo yanayoongozwa na jaji mstaafu wa mahakama ya rufaa, jaji salimu masati.
Jaji kiongozi wa mahakama nchini Eliezer Feleshi akizungumza kwenye mafunzo hayo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments