WAZIRI SIMBACHAWENE AITAKA POLISI KUKAA MGUU SAWA UCHAGUZI MKUU, AIPONGEZA RUFIJI KUSAMBARATISHA WAHALIFU

Na Mwandishi Wetu, MOHA, Rufiji.

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, George Simbachawene amelitaka Jeshi la Polisi kudhibiti vurugu zozote au uvunjifu wa sheria hasa katika kipindi hiki nchi inapoelekea katika uchaguzi mkuu.

Amewataka muda wote wawe tayari kwa kujipange vizuri na pia intelejensia wahakikishe kila kinachotekea katika jamii wanakijua ili kuhakikisha nchi inakua salama na uchaguzi umalizike salama.

Akizungumza na Viongozi Wakuu wa Mkoa wa Kipolisi Rufiji, Mjini Ikwiriri leo, wakati alipokuwa safarini akitokea Mkoani Mtwara kuelekea Jijini Dar es Salaam, Simbachawene amewataka Polisi wasije kujisahau na kudhani kuwa wapo salama sana bali muda wote wawe macho kujilinda, kulinda raia na mali zao.

“Msije mkajisahau mkadhani mpo salama sana, hawa watu huvamia pale mnapojisahau ndipo wanafanya hayo mambo. Tunapoelekea kipindi hiki cha uchaguzi  ni vizuri mkawa katika tahadhali, intelejensia ikae vizuri kuhakikisha kila kinachotokea kwenye jamii mnakijua,” alisema Simbachawene.

Aliongeza kuwa, “Mshirikiane na vyombo vingine kudhibiti uhalifu, Serikali ni moja, dola ni moja, Mamlaka ni moja na Amiri Jeshi Mkuu ni mmoja, kwahiyo pale mnapopungukiwa tumia taarifa kutoka kwa wenzenu.”

Pia Simbachawene alilitaka Jeshi hilo lithibiti matukio ya uhalifu kuanzia chini na pia wasilipuuze kwa kuwa tukio likidharauliwa ndipo baadaye linbakuja kuwa kubwa na kuleta matatizo makubwa katika jamii.

“Mdhibiti matukio kuanzia chini, utakuta tukio lina cheni fulani lakini halishughulikiwi, hivyo linazaa lingine na matokeo yake linakua kubwa zaidi, matukio yanayotokea yathibitiwe kwa kiasi cha kutosha ili yasije kuleta madhara makubwa hapo baadaye,” alisema Simbachawene.

Aidha, Waziri huyo aliahidi kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo ukosefu wa ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Rufiji, ambapo atahakikisha anamfikishia ombi Rais Dkt. John Pombe Magufuli aweze kusaidia kuanza kwa ujenzi wa ofisi hiyo.

“Nitamuomba mheshimiwa Rais aone uharaka wa kutupa fedha ya ujenzi wa ofisi, ambayo ni shilingi milioni mia tatu, bila ofisi mnawezaje kufanya kazi, hatuwezi kuwaacha watu kwenye vijumba vyenye joto, itakua ni mateso, tutajitahidi tuweze kufanikisha hili kwa kulifanyia kazi kwa uharaka zaidi,” alisema Simbachawene.

Waziri huyo pia alimpongeza Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo wa kipolisi pamoja na wasaidizi wake, kuhakikisha wanadhibiti uhalifu kwa kiasi kikubwa na sasa eneo hilo lina amani na wananchi wanaendelea na shughuli zao za maendeleo.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo wa Kipolisi, SACP Onesmo Lyanga alisema Mkoa wa Kipolisi Rufiji hali ya usalama imeimarika na Wilaya zote nne za Kiserikali ambazo ni Rufiji, Kibiti, Mkuranga na Mafia zipo salama.

“Mkoa huu wa Kipolisi ulianzishwa mwaka 2017, na mpaka sasa, hali ya uhalifu ni shwari, tunaendelea kufanya misako na doria kupambana na uhalifu mdogo na mkubwa unaofanyika katika Mkoa wa Kipolisi Rufiji,” alisema Lyanga.

Pia Lyanga alimshukuru Waziri huyo kwa kuwatembelea, na kuahidi kuyafanyia kazi maelekezo yote aliyowapa, na wataendelea kufanya kazi kwa weledi muda wote kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama katika Mkoa huo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527