SERIKALI KUAJIRI WATUMISHI WAPYA 44,800 KWA KIPINDI CHA 2019/20

Watumishi 44,800 wataajiriwa katika taasisi za Serikali kwa kipindi cha 2019/20.


Hayo yameelezwa na naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Dk Mary Mwanjelwa jana Jumanne Mei 28, 2019. na kubainisha kuwa ajira hizo zitawalenga Watanzania wenye sifa.

Dk Mwanjelwa alisema kuwa si Serikali pekee ndio inayotakiwa kutoa ajira, hata watu binafsi wanaweza kutoa ajira kwa vijana.

Naibu Waziri huyo alikuwa akijibu swali la mbunge wa Viti Maalum (Chadema), Aida Khenan aliyehoji kama kuna utaratibu wowote wa kuajiri watu waliohitimu vyuo na kukidhi vigezo vya kuajiriwa.

Katika swali la nyongeza mbunge huyo amehoji kwa nini Serikali inaendelea kuweka vigezo vya uzoefu kazini wakati inajua hakuna vijana wenye uzoefu.

Katika majibu yake, Dk Mwanjelwa alisema duniani kote Serikali si mwajiri pekee, akitolea mfano waajiri wengine ambao ni sekta binafsi, mashirika, asasi za kiraia na maeneo mengine.

Kuhusu uzoefu, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Jenister Mhagama alisema wameondoa uzoefu badala yake Serikali imeanzisha kozi maalum kwa wahitimu ambazo husaidia kuwapa ujuzi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527