MCHUNGAJI AONYA WACHUNGAJI KUWA UPANDE WA ADUI


Mchungaji Mwangalizi Mkuu wa makanisa ya Presbyterian Tanzania, Mchungaji Sylvester Ng’welemi   ameonya tabia ya wachungaji kusemana vibaya katika huduma zao, kitu ambacho kinawafanya wawe upande wa adui wao Shetani.

Onyo hilo amelitoa leo tarehe 30.03.2019 alipokuwa katika ibada maalum ya Uzinduzi wa Kanisa la Shekinah Presbyterian tawi la Mbopo. 

Alisema kwamba mojawapo ya changamoto kubwa kwa wachungaji siku hizi ni kuwa wanapoona huduma mpya imeanzishwa katika maeneo yao wanaamua kuiponda na kuiita majina ya ajabu ajabu kama vile “Freemasons.” Je Freemasons ndio wanapaswa kufanikiwa? aliuliza umati mkubwa watu uliokuwa umebanana kwenye jengo jipya la kanisa. Alihoji kwamba “kwa nini wachungaji wanapofanikiwa wapendwa ambao si wa madhehebu hayo huanza kuhoji maswali, kwa nini wasihoji wakati bado maskini?” 


Katika ibada hiyo ambayo ilijumuisha tukio la kuweka wakfu jengo la kanisa ambalo limejengwa kwa mfupi sana kwa ufadhili wa wamissionari kutoka Korea Kusini, Mwangalizi aliwatia moyo wachungaji wa Presbyterian Church Tanzania (PCT) kwamba wanahitaji kusimama imara kwa kufundisha ukweli, na kwamba fedha zinazotumika kujenga makanisa haya wazione kuwa ni za thamani kwa sababu watu wale wanaotoa wana haki ya kutumia pesa hizo kwa ajili ya mambo mengine

 “ kanisa la PCT linasimama katika ukweli, na miujiza inatendeka, kama ukitaka kuhakikisha njoo kanisani kwangu” alisisitiza mchungaji huyu ambaye ni mchungaji kiongozi wa kanisa la Efatha Presbyterian la Kigamboni-Mjimwema. 

Alihoji kwamba “kwa nini watu wanahoji kujengwa kwa jengo hili kwa haraka? je ni kweli kwamba Mungu wetu hawezi? kwa nini watu wanapenda tukae kwenye kanisa la makuti tu? je sisi tusiabudu kwenye makanisa ya kisasa kama hili? mtu anapoamua kusema vibaya juu ya kanisa hili, maana yake ameamua kuwa upande wa adui, na jambo hili ni hatari sana kwa sababu ni laana kwao.


Vile vile katika ibada hii kuliambatana na zoezi la kutoa Msaada wa kimasomo (Scholarship) kwa watoto wanaoishi katika mazingira magumu. watoto hamsini walipokea vyeti vya msaada kwa ajili ya kupokea sare za shule. 

Aliyesimamia utoaji wa msaada, ambaye ni mchungaji Daniel John Seni wa makanisa ya Shekinah Presbyterian alisisitiza kwamba ni lazima Watanzania tuendane na kasi ya serikali ya awamu ya tano. Alisisitiza kwamba “kanisa letu linaungana na serikali ya awamu ya tano kwa kutoa msaada wa kimasomo.”


Katika sherehe hii ambayo ilihudhuriwa na wachungaji mbalimbali wa makanisa ya Presbyterian, wachungaji wa makanisa jirani pamoja na kwaya mbalimbali; pia Mwangalizi aliwakaribisha wachungaji wote kwa ajili ya kumsimika rasmi, Mchungaji Zakayo Nashoni kwa ajili ya kutumika rasmi katika kanisa hilo.


Mwangalizi aliwasihi wachungaji kuimarisha umoja miongoni mwao, na kushirikiana na Mchungaji Zakayo Nashoni kwa ajili ya kuleta maendeleo katika eneo la Mbopo na maeneo jirani.

Taarifa hii imetolewa na:
Kitengo cha habari
Shekinah Presbyterian Church (T)
0769080629



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527