HAYA NDIYO MASHTAKA 28 YANAYOMKABILI RAIS WA TFF JAMAL MALINZI


Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi hataweza kutetea nafasi yake hiyo katika Uchaguzi Mkuu uliopangwa kufanyika Agosti 12 mjini Dodoma.


Hiyo inatokana na kushindwa kufika kwenye usaili ulioanza jana na kumalizika kesho kwa kuwa yupo rumande akikabiliwa na kesi.


Mbali ya Malinzi, pia Makamu wa Rais wa Simba, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ aliyekuwa akiwania nafasi ya Makamu wa Rais TFF, pia amepoteza nafasi hiyo kwa kuwa naye yupo rumande.


Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi TFF, Revocatus Kuuli alisema mgombea ambaye atakosa kufika kwenye usaili katika muda huo atakuwa amejiondoa kwenye uchaguzi.


Malinzi, ambaye aliingia madarakani mwaka 2013 alikuwa akitetea kiti chake ambacho kingemfanya kuwa madarakani kwa miaka mingine minne iwapo angechaguliwa.


Jana, Malinzi (57), Katibu Mkuu wake, Mwesigwa Celestine (46) na Mhasibu, Nsiande Mwanga (27) walipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka mbalimbali ikiwamo ya kughushi na kutakatisha fedha dola za Marekani 375,418 (Sh840 milioni).


Malinzi anashtakiwa kwa makosa 28, huku wenzake wakishtakiwa kwa makosa yasiyozidi manne.


Walisomewa mashtaka hayo na Wakili wa Serikali, Nassoro Katuga ambaye alidai kuwa katika shtaka la kwanza, Malinzi na Mwesigwa, Juni 5, 2016 wakiwa Dar es Salaam kwa nia ya kudanganya, walighushi nyaraka zinazoitwa Maazimio ya Kamati ya Utendaji (Executive Committee Resolution) wakionyesha Kamati ya Utendaji ya TFF imebadili mtia saini wa akaunti ya benki ya TFF, Edgar Leonard Masoud kuwa Nsiande Isawafo Mwanga wakati wakijua si kweli.


Katika shtaka la pili, Wakili Katuga alidai kuwa Septemba Mosi, 2016 katika benki ya Stanbic, tawi la Kinondoni, Mwesigwa aliwasilisha nyaraka hiyo ya kughushi.


Katika shtaka la tatu, inadaiwa kuwa Desemba 17, 2013 katika ofisi za TFF, Malinzi alighushi risiti namba 308 ya Novemba 6, 2013 akionyesha ameikopesha TFF dola za Marekani 9,300 (Sh19 milioni) wakati akijua si kweli.


Katika shtaka la nne, Malinzi anadaiwa kuwa Desemba 17, 2013 katika ofisi ya TFF, alighushi risiti namba 322 akionyesha ameikopesha TFF dola za Marekani 10,000 (Sh20 milioni) wakati si kweli.


Shtaka la tano, Malinzi anadaiwa kuwa Desemba 17, 2013 katika ofisi ya TFF alighushi risiti namba 323 akionyesha ameikopesha TFF dola za Marekani 18,000 (Sh37 milioni).


Katuga alidai kuwa katika shtaka la sita, Desemba 17, 2013, Malinzi kwenye ofisi hiyo ya TFF alighushi risiti namba 324 akionyesha ameikopesha TFF dola 5,000 (Sh10 milioni).


Katika shtaka la saba, Malinzi anadaiwa kuwa Desemba 17, 2013 katika ofisi ya TFF alighushi risiti namba 325 akionyesha ameikopesha TFF dola 1,032 (Sh2 milioni) wakati akijua si kweli.


Katika shtaka la nane, Katuga alidai kuwa Machi 26, 2014, Malinzi alighushi risiti namba 1956 akionyesha ameikopesha TFF dola za 40,000 (Sh84 milioni).


Wakili huyo wa Serikali alidai katika shtaka la tisa kuwa, Machi 13, 2014, Malinzi alighushi risiti namba 1957 akionyesha ameikopesha TFF dola 5,000 (Sh 10 milioni).


Aliendelea kudai kuwa katika shtaka la 10, Mei 13, 2014, Malinzi alighushi risiti namba 1624 akionyesha ameikopesha TFF dola 40,000 (Sh84 milioni).


Katika shtaka la 11, Katuga alidai kuwa Mei 16, 2014, Malinzi alighushi risiti namba 1634 akionyesha ameikopesha TFF dola 10,000 (Sh20 milioni).


Shtaka la 12, Malinzi anadaiwa kuwa Julai 11, 2014, alighushi risiti namba 1860 akionyesha kuwa ameikopesha TFF dola 15,000 (Sh30 milioni).


Katika shtaka la 13, Malinzi anadaiwa kuwa Julai 11, 2014 alighushi risiti namba 1861 akionyesha ameikopesha TFF dola 3,000 (Sh6 milioni).


Katika shtaka la 14, inadaiwa kuwa Julai 15, 2014, Malinzi alighushi risiti namba 1863 akionyesha kuwa ameikopesha TFF dola 14,000 (Sh28 milioni).


Iliendelea kudaiwa katika shtaka la 15 kuwa, Julai 15, 2014, Malinzi alighushi risiti namba 1866 akionyesha ameikopesha TFF dola 4,000 (Sh8 milioni).


Katuga alidai katika shtaka la 16, Malinzi anadaiwa kuwa Julai 25, 2014 , alighushi risiti namba 1876 akionyesha ameikopesha TFF dola 1,000 (Sh2 milioni).


Katika shtaka la 17, wakili huyo alidai kuwa Agosti 19, 2014, Malinzi alighushi risiti namba 1890 akionyesha ameikopesha TFF dola 5,000 (Sh10 milioni).


Kwenye shtaka la 18, Katuga alidai kuwa Oktoba 11, 2014, Malinzi alighushi risiti namba 1568 akionyesha ameikopesha TFF dola 1,200 (Sh2.4 milioni) wakati akijua si kweli.


Shtaka la 19, Malinzi anadaiwa kuwa Agosti 17, 2015 alikula njama ya kughushi risiti namba 1511 akionyesha kuwa ameikopesha TFF dola 5,000 (Sh 10 milioni).


Mwendesha Mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Leonard Swai akisoma shtaka la 20, alidai kuwa Julai 22, 2015, Malinzi alighushi risiti namba 2981 akionyesha kuwa ameikopesha TFF dola 2,000 (Sh4 milioni).


Swai akisoma shtaka la 21, alidai kuwa Mei 9, 2016, Malinzi alighushi risiti namba 832 akionyesha ameikopesha TFF dola 7,000 (Sh14 milioni) wakati akijua si kweli.


Katika shtaka la 22, Swai alidai kuwa Juni 16, 2016, Malinzi alighushi risiti namba 931 akionyesha ameikopesha TFF dola 10,000 (Sh20 milioni).


Inadaiwa katika shtaka la 23, kuwa Agosti 2, 2016, Malinzi alighushi risiti namba 947 akionyesha kuwa ameikopesha TFF dola 1,000 (Sh2 milioni).


Akiendelea kusoma hati ya mashtaka, Swai alidai katika shtaka la 24 kuwa Septemba 19, 2016, Malinzi alighushi risiti namba 1029 akionyesha ameikopesha TFF dola 1,000 (Sh 2 milioni).


Swai katika shtaka la 25, alidai kuwa Septemba 22, 2016, Malinzi alikula njama ya kughushi risiti namba 1071 akionyesha kuwa ameikopesha TFF dola 15,000 (Sh30 milioni).


Kwenye shtaka la 26, ilidaiwa kuwa kati ya Septemba Mosi na Oktoba 19, 2016 washtakiwa Malinzi, Mwesigwa na Mwanga kwa pamoja, walitakatisha fedha kiasi cha dola 375,418 huku wakijua fedha hizo ni zao la kughushi.


Katika shtaka la 27, Swai alidai kuwa Malinzi na Mwesigwa katika kipindi hicho cha Septemba Mosi na Oktoba 19, 2016 katika benki ya Stanbic, tawi la kati la Kinondoni walijipatia dola 375,418 wakati wakijua fedha hizo zimetokana na kughushi.


Katika shtaka la 28, Mwanga anadaiwa kuwa kati ya Septemba Mosi na Oktoba 19, 2016 katika ofisi ya TFF aliwasaidia Malinzi na Mwesigwa kujipatia dola 375,418 kutoka benki ya Stanbic huku akijua upatikanaji wake umetokana na kughushi.


Baada ya washtakiwa hao kusomewa mashtaka hayo yanayowakabili Wakili wa Serikali Mwandamizi, Kishenyi Mutalemwa aliiambia Mahakama kuwa upelelezi bado haujakamilika.


Jopo la mawakili wa utetezi likiongozwa na Jerome Msemwa na Aloyce Komba liliiomba Mahakama iwapatie dhamana washtakiwa hao lakini Mutalemwa na mawakili wenzake wa Serikali waandamizi, Christopher Msigwa na Pius Hilla walipinga dhamana kwa washtakiwa hao kwa madai kuwa mashtaka ya kutakatisha fedha yanayowakabili hayana dhamana.


Hakimu Wilbard Mashauri anayesikiliza kesi hiyo, aliiahirisha hadi Jumatatu ijayo atakapotoa uamuzi kama washtakiwa hao watapata dhamana hivyo, walipelekwa rumande.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments