POLEPOLE : KINANA HAJAJIUZULU AU KUANDIKA BARUA YA KUJIUZULU

Chama cha Mapinduzi (CCM), kimesema Katibu Mkuu wake, Abdulrahman Kinana hajahudhuria vikao vya kamati kuu na halmashauri kuu kwa kuwa aliomba udhuru wa kihali kwa kuwa anauguza ndugu yake wa karibu wa familia.


"Ndugu yetu Kinana anauguza ndugu yake wa karibu, tumwombee apone lakini Kinana alishiriki vyema kikao cha Sekretarieti. Kinana hajajiuzulu au kuandika barua ya kujiuzulu," amesema Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole.


Chama hicho pia kimetangaza kuwachukulia hatua kali makada wake watakaobainika kukiuka utaratibu wa uchaguzi wa ndani wa chama hicho.


Polepole amesema hayo leo Jumamosi alipozungumza na waandishi wa habari katika ofisi ndogo za chama hicho Lumumba jijini hapa akitoa taarifa ya vikao vya juu vilivyoanza juzi Ikulu ya Dar es Salaam. Amesema Mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli amesema vikao hivyo vimepitisha majina ya wagombea wa uenyekiti ngazi ya wilaya.


Amesema kati ya wilaya 161 za kiserikali ambazo ni sawa na za kichama, kikao cha Kamati Kuu na Halmashauri Kuu iliyoketi leo Jumamosi imezuia uchaguzi katika wilaya sita.


Amezitaja wilaya hizo kuwa Moshi Mjini, Siha, Hai na Makete kwa sababu waliojitokeza kugombea wameonekana kuwa watu hatarishi kwa chama hicho na uchaguzi utatangazwa baadaye.


Wilaya za Musoma Mjini na Musoma Vijijini zitarudia baada ya kutenganishwa kutoka wilaya moja na kuwa mbili.


"Chama hakitasita kuwachukulia hatua kali ikiwemo kufuta uchaguzi au kuwafukuza uanachama wale wote watakaobainika kutozingatia maadili na kanuni za chama chetu," amesema Polepole.


Amesema Halmashauri Kuu imetoa onyo kali kwa wanachama wa Zanzibar walioanza kampeni za uchaguzi mkuu ikisema muda bado na wakiendelea watachukuliwa hatua.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
أحدث أقدم