Diwani wa CHADEMA Atiwa Mbaroni Kwa Tuhuma za Kumbaka Binti wa Miaka 14 Gesti


Diwani wa Mtibwa wilayani Mvomero, Lucas Edward (38) maarufu Mwakambaya anashikiliwa na Polisi Mkoa wa Morogoro kwa tuhuma za kumbaka binti wa miaka 14, mkazi wa Turiani kwenye nyumba ya kulala wageni.


Kamanda wa Polisi mkoani Morogoro, Ulrich Matei alisema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa Mei 29 saa 12 jioni kwenye nyumba hiyo iliyopo Mtaa wa Sultan, Manispaa ya Morogoro.


Matei alisema polisi walipata taarifa kutoka kwa msiri wao kwamba katika nyumba hiyo, kuna mtu ameonekana akiwa na binti mdogo, hivyo askari walifuatilia nyendo zake na kumkamata.


Alisema askari baada ya kufika kwenye nyumba hiyo, walimkuta mtuhumiwa huyo akiwa na binti huyo chumba namba 108.


Alisema uchunguzi wa kitabibu unaendelea kuthibitisha tuhuma hizo.


Akizungumza kwa simu, Katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Wilaya ya Mvomero, Mrisho Ramadhan alithibitisha kukamatwa kwa diwani huyo na kwamba mpaka sasa hajafahamu ni kwa tuhuma gani.


Ramadhan alisema kwa sasa wao kama viongozi wa chama wanafuatilia kujua tuhuma na ameomba uongozi wa Chadema Mkoa kufuatilia zaidi na kwamba, atatoa taarifa baada ya kufahamu kwa undani.


“Ni kweli nimesikia mheshimiwa kakamatwa huko mjini Morogoro, sijajua kosa nimewaomba viongozi wa Mkoa Chadema kufuatilia nitatoa maelezo baadaye,” alisema Ramadhan.


Alisema baada ya kupata undani wa tukio hilo, atatoa taarifa ili kujulisha umma kilichotokea.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
أحدث أقدم