News Alert! MASELE ASHINDA KWA KISHINDO UBUNGE SHINYANGA MJINI,UPINZANI WAPINGA,WANANCHI WAPIGWA MABOMU,YA RAIS MPAKA KESHO



Mheshimiwa Stephen Masele akiwashukuru wakazi wa Shinyanga kwa kumchagua kuwa mbunge katika uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 25,2015-Picha na Kadama Malunde-Malunde1 blog

*********
Mgombea ubunge katika jimbo la Shinyanga mjini kwa tiketi ya Chama cha Mapinduzi (CCM), Stephen Masele ametangazwa kuwa mshindi katika uchaguzi mkuu baada ya kupata kura 35,858 na kumshinda mpinzani wake wa karibu Patrobas Katambi wa CHADEMA aliyepata kura 31,027.



Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa leo na msimamizi wa uchaguzi katika jimbo la Shinyanga mjini, Lewis Kalinjuna mgombea ubunge kwa tiketi ya chama cha ACT – Wazalendo Nyangaki Shilungushela alipata kura 481 huku mgombea wa chama cha APPT Maendeleo, Elisiana Tambwe akiambulia kura 78 kati ya kura zote 67,444 zilizopigwa.



Hata hivyo wagombea wote kutoka vyama vya upinzani wamepinga matokeo hayo baada ya msimamizi wa uchaguzi kukataa kurejea kuhesabiwa upya kwa baadhi ya masanduku ya kura yaliyoonesha kuwa na utata ikiwemo ya kituo cha Town Shule ya msingi yaliyodaiwa kuwa na idadi kubwa ya kura zilizopigwa ikilinganishwa na idadi ya wapiga kura.



Kutokana na hali hiyo mgombea ubunge wa CHADEMA, Patrobas Katambi amekataa kuyatambua matokeo hayo na kuahidi kufungua kesi mahakamani ya kupinga uchaguzi huo aliodai ulitawaliwa na rushwa na nguvu kubwa ya jeshi la polisi ikidaiwa vitisho vyao vilikuwa na lengo la kuwasaidia wagombea wa CCM kushinda.



Katika hatua nyingine msimamizi wa uchaguzi amekataa kutangaza matokeo ya kura za urais ambapo alisema zoezi la kuhesabu kura za rais litafanyika kesho na matokeo yatatangazwa siku hiyo kwa kile alichodai inatokana na vurugu zilizotokea kabla na baada ya kutangazwa kwa matokeo ya ubunge.



Kabla ya kuanza kwa zoezi la kuhesabu kura msimamizi wa uchaguzi aliwakaribisha wagombea wa vyama vyote kuzungumzia kuhusu uchaguzi ambapo wagombea wa vyama vya upinzani wakiongozwa na Mgombea wa Chadema Patrobas Katambi na Elisiana Tambwe walieleza kutoridhishwa na mwenendo mzima wa uchaguzi na kudai kuwa mgombea wa CCM amekuwa akitoa rushwa waziwazi bila kuchukuliwa hatua na vyombo vinavyohusika.



Kufuatia hali hiyo msimamizi wa uchaguzi alianza kusoma matokeo ya vituo vyote 275 vya uchaguzi,na wakati zoezi linaendelea wagombea wa upinzani walitoka nje ya chumba cha kuhesabia na kutangazia matokeo huku mgombea wa Chadema akisindikizwa na wafuasi wa chama chake kuelekea kwenye ofisi za chama hicho.



Hata hivyo jeshi la polisi halikuingilia kitendo hicho huku zoezi la kuhesabu kura kituo baada ya kituo na wakati zoezi hilo linaendelea wananchi walianza kurusha mawe kwenye chumba cha kuhesabia kura ndipo polisi wakaanza kufyatua mabomu ya machozi katika kukabiliana na vurugu za wafuasi wa CHADEMA waliokuwa wakipinga matokeo hayo hasa pale msimamizi alipogoma kurudia kuhesabu kura za vituo vilivyokuwa na mashaka hali iliyosababisha kufungwa kwa maduka yote ya biashara mjini humo.



Taarifa kutoka majimbo ya Kishapu (Suleiman Nchambi), Solwa (Ahmed Salum), Kahama (Jumanne Kishimba), Msalala (Ezekiel Maige) na Ushetu ( Elias Kwandikwa) zilidai wagombea ubunge wote wa CCM walikuwa wameshinda katika uchaguzi huo.

Na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
أحدث أقدم