BARAZA LA VYAMA VYA SIASA TANZANIA LASOGEZA MBELE TAREHE YA KUTAFUTA SULUHU YA UKUTA

Baraza la Vyama vya Siasa nchini limesogeza tarehe ya mkutano wa kutafuta suluhu ya operesheni Ukuta iliyotarajiwa kufanyika Septemba 1,2016 ,kutoka Agosti 30 hadi Septemba 3 mwaka huu.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam Kaimu Mwenyekiti wa baraza hilo Vuai Ally Vuai alisema mkutano huo umesogezwa hadi tarehe 3 na 4 Septemba,2016.

“Kamati ya uongozi leo tumekutana tena ili kufanya maandalizi ya mkutano tuliopanga kuufanya tarehe 30 na 31 mwezi huu.

“Tumepitia list (orodha) ya wahudhuriaji, tumegundua siku zilizobaki kufikia mkutano zisingetosha . Tumeamua kuusogeza mbali hadi tarehe 3 na 4, Septemba mwaka huu ili mkutano uwe wa ufanisi,” alisema Vuai.

Aidha, baadhi ya agenda zilizotarajiwa kujadiliwa katika mkutano huo ni masuala ya amani na utulivu nchini pamoja na hali ya siasa kwa sasa.

Waandishi wa habari walipohoji kwa nini baraza hilo lisifanye mkutano huo katika tarehe zilizopangwa awali ili kutoa nafasi kwa wajumbe kujadili suala la operesheni Ukuta ambayo imezua mabishano makali ya kisheria na kikatiba kati ya serikali na Chadema, Cons Akitandi, Mwenyekiti wa fedha wa baraza hilo alisema “kwanza ifahamike hatukutani kwa ajili ya Septemba Mosi.”

“Upo utaratibu wa kikanuni kwamba baraza lina vikao vya kila baada ya miezi mitatu na vikao vya dharula. Haki haitapatikana katika mazingira ya shari, wajumbe wanapaswa kutumia njia ya majadiliano na maridhiano katika kufikia mwafaka,” alisema Akitandi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527