TBS YAONYA WAFANYABIASHARA WANAOKIUKA TARATIBU ZA UINGIZAJI WA BIDHAA ZA MABATI NCHINI

Kaimu Mkurugenzi Mkuu ( TBS), Bw. David Ndibalema akiongea na waandishi wa habari alipotembelea ghala la kampuni ya URHOME inayoagiza na kusambaza bidhaa za mabati kutoka nchini China. Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara kutoka Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara Bw. Christopher Mramba akizungumza na waandishi wa habari leo alipotembelea ghala la kampuni ya URHOME inayoagiza na kusambaza bidhaa za mabati kutoka nchini China. Mkurugenzi wa Utekelezaji na Uzingatiaji wa Sheria TBS, Dkt. Candida Shirima akizungumza na waandishi wa habari alipotembelea ghala la kampuni ya URHOME inayoagiza na kusambaza bidhaa za mabati kutoka nchini China. Meneja wa uthibiti wa Shehena zinazoingia na kutoka nchini Mhandisi Saidi Mkwawa akizungumza na waandishi wa habari alipotembelea ghala la kampuni ya URHOME inayoagiza na kusambaza bidhaa za mabati kutoka nchini China. Mabati yaliyo chini ya kiwango mali ya Kampuni ya URHOME yaliyozuiwa na TBS kwa ajili ya uteketezaji, maeneo ya Sokota, wilayani Temeke, Dar es Salaam mapema leo.

***************************

NA EMMANUEL MBATILO, DAR ES SALAAM

SHIRIKA la Viwango Tanzania limeiandikia barua kampuni ya uagizaji na usambazaji wa mabati nchini URHOME Company Limited kuhakikisha ndani ya siku tatu wamewapatia taarifa ya mabati 2176 kati 125280 yapo wapi baada ya kufanyiwa ukaguzi na kugundulika hayajakidhi viwango.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Septemba 30 Jijini Dar es Salaam, Meneja wa uthibiti wa Shehena zinazoingia na kutoka nchini Mhandisi Saidi Mkwawa amesema Kampuni hiyo baada ya kuingiza nchini mabati hayo, TBS ilichukua sampuli na kuzipeleka kwenye maabara ya Shirika ili kubaini kama zimeweza kukidhi viwango stahiki kwa mujibu wa sheria .

Aidha baada ya matokeo ya uchunguzi ilibainika kwamba mabati kutoka kampuni hiyo yameshindwa kukidhi viwango vya ubora vilivyotarajiwa, kama ilivyo taratibu za sheria, kulikuwa na njia mbili aidha kurudisha au kuteketeza na mteja alikubaliana na njia ya kuteketeza na zoezi la uteketezaji lilianza.

"Wakati tukiendelea kuteketeza ambapo mabati hayo awali yalikuwa 125280 tukaja tukabaini mabati 2176 hayapo na taratibu za kisheria zimeshaanza". Amesema

Pamoja na hayo Mhandisi Mkwawa amesema watahakikisha mabati yote yanapatikana na zoezi la uteketezaji litaendelea sambamba na mengine.

Nae Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TBS, Bw.David Ndibalema amewahimiza wafanyabiashara na waingizaji wabidhaa kutumia vizuri vibali vya masharti kwa kuhakikisha wanazingatia yale masharti ambayo yamewekwa wakati wa kutoa vibali hivyo.

masharti yenyewe ni kwamba kama mzigo bado upo chini ya uchunguzi mzigo huo hautakiwi usambazwe, kuuzwa au kutumiwa kwa njia yoyote ile na tutaendelea kuchukua hatua za kisheria kwa wale ambao wanakiuka akiwemo huyu ambaye ameingiza huu mzigo wa mabati ambayo yamegundulika yapo chini ya viwango

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Maendeleo ya Biashara Wizara ya Uwekezaji,Viwanda na Biashara Bw.Christopher Mramba amesema wamesikitishwa na tukio hilo na kukemea ukiukwaji wa masharti ya vibali vinavyowekwa na serikali na kuzingatia sheria na kuendelea kujenga utamaduni wakuzingatia masharti ya ubora wa bidhaa na kamwe serikali haitaacha soko la Tanzania liwe dampo kuweka bidhaa zisizo na ubora.

"Tutaendelea kushirikiana na vyombo vya serikali kufuatilia bidhaa ambazo zimeingia sokoni kinyume na sheria na kuchukua hatua stahiki za kisheria na nitoe wito kwa wafanyabiashara wote nchini kuzingatia uaminifu na matumizi mazuri ya fursa zinazotolewa na serikali za kuweka mazingira wezeshi ya biashara ikiwemo hii fursa ya kutoa kibali cha masharti maalumu ya kutoa mzigo bandarini ili bandari yetu iendelee kuwa na ufanisi unaotakiwa na pasiwe na msongamano ili biashara nyingine ziwezee kufanyika". Amesema

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

1/Post a Comment/Comments

Post a Comment