MAFURIKO YAUA WATU 10

Watu kumi wamepoteza maisha nchini Uganda kufuatia mafuriko makubwa mashariki kwa taifa hilo la ukanda wa Afrika Mashariki, shirika la Msalaba Mwekundu lilisema Jumapili.

Mvua kubwa ilisababisha mito kufurika na maji kusambaa hadi katika maboma ya watu na barabara huku Red Cross ikielezea uwezekano wa idadi ya maafa kuongezeka.

 Waliofariki ni waathiriwa wa mvua kubwa iliyohushudiwa usiku wa Jumamosi katika wilaya za Kapchorwa na Mbale. Video zinaonyesha wakaazi waliojawa na hofu wakikimbilia usalama wao huku viwango vya maji vikiongezeka katika kijiji kimoja na kuangusha nyumba na migomba ya ndizi.

Kwa mujibu wa kamishna wa Mbale Ahamada Waashaki, mwanajeshi ni mmoja wa watu waliongamizwa na mafuriko hayo. 

"Watu wengi hawajulikani waliko na wanahofiwa kuaga dunia. Kuna uharibifu mkubwa. Barabara zimezibwa, nyumba kumezwa kwa sababu ya mvua kubwa iliyoanza usiku wa jana (Jumamosi) hadi asubuhi hii (Jumapili)," Ahamada Waashaki aliambia shirika la habari la AFP.

 Waziri Mkuu Robinah Nabbanja alitembelea Mbale, eneo ambalo linapatikana takriban kilomita 300 mashariki mwa jiji kuu la Kampala.

 "Polisi na wanajeshi wa majini watafika kusaidia katika uokoaji na kutafta miili ya walioaga dunia tunapotoa msaada kwa wale walioathirika," ofisi ya waziri mkuu ilisema. 

AFP inaripoti kuwa wanahabari wawili waliiambia kuwa waliona miili ikielea katika maji hayo yaliyojaa matope kabla ya kuopolewa na polisi. Magari kadhaa pia yalisombwa pamoja na vitu vya nyumbani wakaazi wakikimbilia maeneo ya juu kwa usalama wao.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments