SERIKALI YAZIHAKIKISHIA KAMPUNI ZA UFARANSA MAZINGIRA SALAMA UWEKEZAJI

Na Mwandishi Wetu, Dar
Tanzania imezihakikishia Kampuni za Kifaransa kuwa mazingira ya biashara na uwekezaji ni salama na kuwasihi kuwekeza kwa wingi hapa nchini.

Akiongea na Waandishi wa Habari mara baada ya kumalizika kwa kongamano lililowakutanisha Mawaziri wa Kisekta, wafanyabiashara na wawekezaji kutoka Ufaransa Jijini Dar es Salaam, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) amesema Serikali imewahakikishia wafanyabishara na wawekezaji wa kampuni za Kifaransa kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inajenga na inaendelea kuboresha mazingira rafiki ya uwekezaji kwa kuondoa kero mbalimbali zilizokuwa zinawakabili wawekezaji hapa nchini.

“Serikali ya Awamu ya Sita iko serious….. na tuna azma kubwa ya kuhakikisha kwamba tunajenga mazingira rafiki ya kuweza kuwekeza na kuondoa kero zote ambazo zimekuwa zinajitokeza….na makampuni mengine yameeleza hizo kero lakini tunafurahi kuona kero hizo tayari zimeanza kuondolewa,” amesema Balozi Mulamula

Balozi Mulamula ameongeza kuwa Wafaransa wamekuwa na uhusiano mzuri na Tanzania kwa muda mrefu na hivi sasa wamekuwa na shauku ya kufanya biashara na kuwekeza kwa wingi hapa nchini…..ambapo takwimu zinaonesha watalii kutoka Ufaransa kuja Tanzania kila mwezi ni zaidi ya watalii 7000 wanaokuja kutembelea vivutio mbalimbali hapa nchini, hivyo ni changamoto kwetu kuchangamkia fursa hii adhimu.

Kwa upande wake, Waziri wa Biashara za Kimataifa na Uwekezaji wa Ufaransa, Mhe. Franck Riester amesema Ufaransa inatambua jitihada zinazofanywa na Serikali ya Tanzania ikiwa ni pamoja na kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji mambo ambayo pia yanatiliwa mkazo na serikali ya Ufaransa.

“Ufaransa imedhamiria kuongeza ushirikiano na Tanzania na kama mlivyoshuhudia leo tumeanzisha safari za ndege za moja kwa moja kutoka Paris hadi Zanzibar ambao ulisimama tangu mwaka 1974, huu ni mwanzo mzuri” amesema Mhe. Riester  

Mhe. Riester ameongeza kuwa wataendelea kuwaeleza na kuwahamasisha wafanyabiashara na wawekezaji wa Ufaransa juu ya fursa mbalimbali zinazopatika Tanzania ikiwemo katika sekta ya Nishati, Utalii, Viwanda, Usafirishaji pamoja na Uwekezaji ili kuja kuwekeza na kukuza ucbumi wa pande zote mbili.

Mawaziri wa Kisekta waliohudhuria kongamano hilo ni Waziri wa mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb), Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro (Mb), Waziri wa Nishati, Mhe. January Makamba (Mb) Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhe. Prof. Makame Mbarawa (Mb) Waziri wa Uwekezaji – Zanzibar Mhe. Mudrick Soraga, Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Prof. Kitila Mkumbo (Mb) na Waziri wa Ofisi ya Rais Uwekezaji Mhe. Geoffrey Mwambe.

Kampuni zilizoshiriki katika kongamano hilo ni pamoja na; CMA-CGM, Bolloré, Airbus, Thales, Lagardére, Total, Chama cha Wafanyabiashara wa Ufaransa-Tanzania, Engie pamoja na Maurel & Prom.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments