MUHIMBILI WATOA TAARIFA KIFO CHA MZEE MAJUTO

Msanii wa vichekesho nchini Amri Athuman maarufu King Majuto, amefariki leo Jumatano Agosti 8, 2018 saa mbili kamili usiku katika hospitali ya taifa ya Muhimbili ambako alilazwa tangu tarehe 31 Julai, 2018.

Taarifa za msiba huo wa nguli wa maigizo zimethibitishwa na Afisa habari wa Muhimbili Aminiel Eligaisha ambapo amesema Mzee Majuto amefariki akiwa anaendelea na matibabu ambayo aliyaanza Julai 31, mwaka huu baada ya jitihada za madaktari kuokoa uhai wake kushindikana.

''Hali yake ilibadilika majira ya saa tisa alasiri ya leo hivyo kuhamishwa kutoka jengo la Sewahaji kwenda ICU. Ilipofika saa 1.30 jioni hii hali yake ilibadilika zaidi na madaktari walijitahidi kuokoa maisha yale bila mafanikio. Ilipofika saa mbili alikata roho'', amesema.

Mzee Majuto alianza kuumwa muda mrefu akisumbuliwa na tatizo la nyonga ambapo mapema mwezi Mei alipelekwa nchini India kwaajili ya matibabu kabla ya kurejea nchini mwezi Juni ambapo alifikia Muhimbili lakini baadae alipata nafuu na kwenda nyumbani kabla ya kurudishwa tena Muhimbili baada ya hali yake kubadilika.

Mkongwe huyo alitangaza kustaafu kuigiza baada ya kutoka India lakini atakumbukwa kwa kazi zake nyingi za kuchekesha ambazo alizifanya kwa uhodari mkubwa na kuwavutiwa mashabiki wengi.

Marehemu Majuto alizaliwa mwaka 1948 mkoani Tanga na alianza maisha kwa kujishughulisha na shughuli za kilimo kabla ya kuingia kwenye sanaa ya maigizo ambayo ilimpatia umaarufu. Tutaendelea kukupatia taarifa na taratibu za mazishi na msiba kwa ujumla. 

Bwana alitoa Bwana ametwaa. Pumzika kwa amani mzee Majuto.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527