TRA YATISHIA KUUZA MAKONTENA YA PAUL MAKONDA

Mamlaka ya Mapato (TRA), imetangaza kusudio la kupiga mnada kontena 20 za Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, ikiwa atashindwa kuzilipia ushuru na kuzichukua ndani ya siku 30 kuanzia Jumatatu.

Kontena hizo za Makonda ambazo zimesubiri utaratibu wa kuzitoa TRA kwa zaidi ya siku 90 zinazokubalika kwa mujibu wa sheria za kodi, zimesheheni samani za ndani na ofisini.

Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi wa TRA, Richard Kayombo, jana alisema kuwa kwa kawaida bidhaa zote zinapoagizwa na kufika bandarini zinatakiwa kuondolewa ndani ya siku 90.

Kayombo alisema inapotokea muda huo ukapita bila wahusika kuondoa mizigo yao, hujulishwa na mamlaka hiyo kwa kupewa notisi ya siku 30 ili waondoe.

Kwa mujibu wa tangazo la TRA lililotoka kwenye vyombo vya habari Jumatatu, Mamlaka hiyo imetoa notisi ya siku 30 kwa wateja nane akiwamo "Paul Makonda" ambao mizigo yao imekaa bandarini zaidi ya muda unaotakiwa.

Katika tangazo hilo, Kamishna wa Idara ya Kodi ya Ushuru wa Forodha na Bidhaa, ametoa siku 30 kwa wamiliki wa mali mbalimbali zilizopo katika ghala la TRA kwenda kuzichukua la sivyo baada ya muda huo zitapigwa mnada kwa mujibu wa sheria na utaratibu wa ushuru wa forodha.

Kayombo alisema kuwa, mzigo unapopitiliza muda wa kukaa bandarini, TRA huwakumbusha wahusika kwa kuwapa notisi kama ya siku hiyo.

"Tumetoa tangazo hili ili kontena ambazo ziko bandarini ambazo zimepitiliza siku 90 wahusika waende kuziondoa; wasipotekeleza ndani ya muda tuliowapa tutazipiga mnada kwa mujibu wa sheria," alisema.

Kayombo alisema nyaraka za bidhaa hizo ziko sawa tatizo ni muda wa kuziondoa bandarini hapo ndiyo haujafuatwa.

"Siwezi kusema kama wameshindwa kulipa kodi au la lakini hata ikitokea bidhaa ambazo zina msamaha wa kodi zimekaa zaidi ya siku zilizowekwa na wamiliki wakapewa notisi bila kutekeleza, muda wa notisi ukiisha bidhaa husika hupigwa mnada na kwenye hili hatuangalii bidhaa zimetoka wapi, ni msaada au sio msaada," alisema Kayombo.

"Bidhaa ikipitiliza siku za kukaa bandarini kwa mujibu wa taratibu, tunatangaza bila kuangalia zimeagizwa na nani, kuna nini ndani yake, zimelipiwa ama hazijalipiwa kama hazijaondolewa bandarini, tunatangaza, ndivyo tulivyofanya."

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527