BABU TALE ATUPWA MAHABUSU MUDA USIOJULIKANA


Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam leo Mei 23, 2018 imemwamuru mkurugenzi wa kampuni ya Tiptop Connections, Hamis Shaban Taletale maarufu Babu Tale, kukaa mahabusu katika kituo cha Polisi akisubiri amri ya kupelekwa kifungoni katika Gereza la Ukonga.

Mahakama hiyo katika uamuzi uliotolewa na Naibu Msajili, Wilbard Mashauri Februari 16, 2018, iliamuru Babu Tale na ndugu yake Idd Shaban Taletale wakamatwe na kupelekwa kifungoni katika gereza la Segerea baada ya kushindwa kutekeleza hukumu yake.

Katika hukumu hiyo iliyotolewa na Jaji Agustine Shangwa Februari 18, 2016, iliwaamuru ndugu hao kumlipa fidia ya Sh250 milioni, Mhadhiri wa Dini la Kiislam Sheikh Hashim Mbonde, kutokana na makosa ya kutumia mahubiri yake kibiashara bila ridhaa yake.

Kutokana na amri hiyo ya kuwakamata, Babu Tale alitiwa mbaroni jana na kupelekwa mahakamani hapo kwa ajili amri ya kumpeleka kifungoni, lakini alilazimika kurudishwa mahabusu Kituo Kikuu cha Polisi kwa kuwa Naibu Msajili aliyetoa amri ya kuwakamata hakuwapo.

Leo amri ya kumrejesha rumande ilitolewa na Naibu Msajili wa mahakama hiyo, Ruth Massam, mpaka Naibu Msajili Mashauri aliyetoa amri ya kuwafunga atakaporejea kutoka Dodoma alikokwenda kikazi.

Kwa kuwa haijulikani ni lini atarejea, Babu Tale atalazimika kukaa mahabusu kwa muda usiojulikana mpaka Naibu Msajili Mashauri atakaporejea.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527