WANAWAKE 27 MBARONI KWA KUKUTWA WAKIFANYA BIASHARA YA UKAHABA 'KUJIUZA'


WANAWAKE 27 wanashikiliwa na Polisi mkoani Tanga wakidaiwa kukutwa wakifanya biashara haramu ya ukahaba katika mitaa ya Chichi Club, Sabasaba na Chuda jijini Tanga.

Watuhumiwa hao wenye umri kati ya miaka 18 na 41, wamekamatwa kwa nyakati tofauti kati ya usiku wa kuamkia Januari 29 na Februari 2 mwaka huu kufuatia operesheni maalum.

 Operesheni hiyo ililenga kuondoa watu wote wanaodaiwa kufanya biashara haramu ya, ukahaba maeneo yasiyo rasmi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tanga, Edward Bukombe, amesema hayo mwishoni mwa wiki akitoa taarifa kwa vyombo vya habari hapa. Alisema, wakati wanawake hao wanakamatwa na askari Polisi, walikuwa wameva nguo za nusu uchi mavazi ambayo hayatakiwi nchini.

“Polisi tuko kwenye operesheni kudhibiti chimbuko la uhalifu kupitia vishawishi vya uhalifu vinavyotokana na hawa changudoa ambao tumebaini ndio wanaotumika sasa kuvuta na kushawishi watu wafanye uhalifu,” alisema.

Alisema wanawake hao, wanatuhumiwa pia kwa kujihusisha na kazi ya kupitisha mihadarati ya aina mbalimbali mkoani na hatua ya kuwaondoa itadhibiti vishawishi na vyanzo vya uhalifu. Kamanda Bukombe alisema watuhumiwa hao watafikishwa mahakamani leo kwa kosa hilo na kwamba operesheni hiyo itakuwa ni endelevu.

IMEANDIKWA NA ANNA MAKANGE - HABARILEO TANGA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527