WANACHAMA WA CHADEMA WAPIGWA MABOMU


Wanachama wa Chadema waliokuwa wanaandamana kuelekea ofisi ya msimamizi wa uchaguzi jimbo la Kinondoni, Aron Kagurumjuli wakiongozwa na mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe wametawanywa kwa mabomu na Polisi.

Akizungumza jana Februari 16, 2018 kabla ya kuhitimisha kampeni za chama hicho zilizofanyika katika viwanja vya Buibui, Kinondoni, Mbowe amesema mpaka sasa mawakala wa chama hicho hawajapewa barua za utambulisho na msimamizi wa uchaguzi.

“Jana nilizungumza na Mkurugenzi wa Uchaguzi (Kailima Ramadhani) nikamweleza kwamba kuna tatizo mawakala wetu hawajapewa barua za utambulisho, akaahidi tungezipata leo asubuhi lakini mpaka sasa hivi saa 12 jioni hatujapata barua hizo,” amesema na kuongeza:

“Kutokana na hali hiyo hivi sasa tukitoka hapa twende kwa msimamizi wa uchaguzi kuchukua barua za utambulisho wa mawakala.”

Wafuasi hao walipofika katika bonde la mto Mkwajuni Polisi walianza kufyatua mabomu ya machozi na kulazimika kutawanyika.
Chanzo- Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527