VIONGOZI WA CHADEMA WAITWA POLISI

Viongozi waandamizi wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wameitwa na jeshi la polisi na kutakiwa kufika jioni ya  Februari 19, 2018.

Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje wa CHADEMA, John Mrema amethibitisha kuwa viongozi waandamizi wa chama hicho wameitwa jana  na kuwa barua hiyo imefika Makao Makuu ya chama leo majira ya saa kumi jioni huku viongozi hao wakitakiwa kufika saa kumi na moja ya jioni kwa Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalum Dar es Salaam katika ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalum Dar es Salaam.

Mrema amesema kuwa viongozi hao walioitwa wameshindwa kufika kituo cha polisi kwa kile alichodai kucheleweshwa kwa barua hiyo kwani imefika saa kumi na dakika 51 na ikisema viongozi hao wafike saa kumi na moja jambo ambalo limeshindikana kutokana na ukweli kwamba viongozi hao wanaishi katika maeneo mbalimbali hivyo isingewezekana kuwapata wote ndani ya dakika tisa. 

"Cha ajabu walikuwa wanawataka viongozi hao saa kumi na moja kamili jioni hivyo kulikuwa na dakika tisa tu wakati viongozi wanaowataka ni wengi na wamesambaa maeneo mbalimbali, hivyo wanasheria wetu wanashughulika kuwajulisha jeshi la polisi juu ya hilo kwa sababu kama Mbunge kama John Heche ni Mbunge wa Tarime, Ester Matiko na Mbunge wa Tarime hawa watu wamesambaa sasa huwezi kuleta barua Makao Makuu halafu utegemee kuwapata saa kumi na moja jioni yaani dakika tisa wawe wamewasili polisi, hivyo Mawakili wetu watawajulisha polisi wale watakaopatikana na kuwajuza wataripoti saa ngapi" alisema Mrema 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527