Picha : WARSHA YA WAVIU WASHAURI MKOA WA SHINYANGA YAFUNGWA..WATEMBELEA HOSPITALI YA MKOA NA KITUO CHA AFYA KAMBARAGE



Kaimu Mratibu wa Kudhibiti Ukimwi mkoa wa Shinyanga Sherida Madanka akizungumza wakati wa kufunga warsha ya siku tatu kwa WAVIU Washauri kutoka halmashauri sita za mkoa wa Shinyanga.

***
Jumla ya WAVIU Washauri 75 kutoka halmashauri sita za wilaya mkoa wa Shinyanga wamepatiwa mafunzo kuhusu namna ya kuwafuatilia wateja waliopotea katika huduma na kuwarudisha kwenye huduma za tiba na matunzo.

Mafunzo yaliyoandaliwa na shirika la AGPAHI kwa ufadhili wa serikali ya Watu wa Marekani kupitia Centres for Disease Control and Preventation (CDC) yalianza Januari 29,2018 na kumalizika Januari 31,2018 katika ukumbi wa Karena Hotel Mjini Shinyanga. 

Akizungumza wakati wa kufunga warsha hiyo na kugawa vyeti vya ushiriki, Kaimu Mratibu wa Kudhibiti Ukimwi mkoa wa Shinyanga Sherida Madanka, aliwataka WAVIU Washauri kujitambua na kutoa elimu kuhusu haki za WAVIU katika jamii. 

Aidha aliwaasa WAVIU Washauri kutunza siri za wateja wanaowahudumia na kuhakikisha wanakuwa viongozi wa kuigwa katika jamii. 

“Ninaamini mtakwenda kutumia elimu mliyopata kuiemilisha jamii, mnatakiwa muwe kioo cha jamii ili wananchi wapate pa kukimbilia, hakikisheni mnatunza siri za watu mnaowahudumia”,alisisitiza Madanka. 

Alitumia fursa hiyo kulipongeza shirika la AGPAHI kwa huduma linalozotoa katika kutekeleza miradi ya Ukimwi huku akibainisha kuwa shirika hilo limekuwa kimbilio la wengi na mdau mkubwa wa masuala ya afya kwa serikali ya Tanzania. 

Nao washiriki wa warsha hiyo walisema jamii inakabiliwa na ukosefu wa elimu sahihi kuhusu masuala ya Ukimwi hivyo kusisitiza elimu hiyo itolewe kwa viongozi wa dini,waganga wa jadi na jamii kwa ujumla. 

Mratibu wa Masuala ya Watoto,Mama na Baba kutoka AGPAHI mkoa wa Shinyanga, Aminael Tesha aliyataja mambo yaliyojiri katika warsha hiyo kuwa ni pamoja na elimu ya ushauri nasaha na kupima VVU, haki za WAVIU, Konga/NACOPHA,shuhuda na uzoefu wa WAVIU, uundaji wa vikundi katika CTC, namna ya kujaza vitabu na fomu za ufuatiliaji na namna ya kuandaa mpango kazi. 

Mbali na washiriki wa warsha hiyo kujifunza kwa nadharia darasani pia walijifunza kwa vitendo ambapo walitembelea Kituo cha afya Kambarage na hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Shinyanga ili kujifunza kwa vitendo huduma mbalimbali zinazotolewa ili wakaboreshe huduma katika CTC zilizopo kwenye maeneo yao. 

Kupitia mafunzo hayo kwa njia ya Matembezi,WAVIU Washauri walijifunza kwa vitendo kuhusu utaratibu mzima wa utunzaji kumbukumbu,mtiririko wa huduma tangu mteja anapoingia hadi anatoka,njia mbalimbali za kukabiliana na wateja watoro na wapitaji,utoaji wa elimu sahihi ya VVU na Ukimwi na matumizi sahihi ya dawa na lishe bora. 

WAVIU Washauri ni watu wanaoishi na maambukizi ya virusi vya Ukimwi na wamejiweka wazi na huru kuwashauri watu wanaoishi na VVU katika nyanja mbalimbali ikiwemo ufuasi mzuri wa dawa,kutoa ushauri nasaha kwa wenzao, kujitolea kufuatilia na kufundisha kwa njia ya ushuhuda wa maisha sambamba na kuhamasisha WAVIU wenzao kujiunga katika vikundi ili kusaidiana na kupunguza unyanyapaa. 

ANGALIA PICHA ZA MATUKIO WAKATI WA KUFUNGA WARSHA YA WAVIU WASHAURI 
Sherida Madanka akilishukuru shirika la AGPAHI kwa kuendelea kushirikiana na serikali katika kupambana na VVU na Ukimwi.
Madanka akiwasisitiza WAVIU Washauri kuwa mfano mzuri wa kuigwa kwa jamii.
WAVIU Washauri wakimsiliza Sherida Madanka.
Sherida Madanka akikabidhi MVIU Mshauri Sospeter Richard cheti cha ushiriki wa warsha hiyo. Kushoto ni Mratibu wa Kudhibiti Ukimwi halmashauri ya wilaya ya Ushetu, Morgan Mwita.
Sherida Madanka akishikana mkono na Agnes John wakati wa zoezi la kugawa vyeti kwa washiriki wa warsha hiyo.
Kulia ni Mariam Wilson akipokea cheti cha ushiriki.
Kulia ni Michael Kabupu akifurahia wakati wa kupokea cheti cha ushiriki.
Kijana Seleman Emmanuel akipokea cheti cha ushiriki.
Katikati ni Mratibu wa Masuala ya Watoto,Mama na Baba kutoka AGPAHI mkoa wa Shinyanga, Aminael Tesha akishikana mkono na mmoja wa washiriki wa warsha hiyo.
Washiriki wa warsha hiyo wakifurahia baada ya warsha kufungwa.
Picha ya pamoja washiriki wa warsha hiyo.
Picha ya pamoja.

PICHA ZA MATUKIO YALIYOJIRI SIKU YA PILI YA WARSHA YA WAVIU WASHAURI 
Mtoa huduma za afya katika kituo cha tiba na matunzo cha hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga Elizabeth Lubasha akitoa maelezo kwa WAVIU Washauri namna wanavyohudumia wateja. Alisema wamekuwa wakihudumia wateja takribani 150 kila siku. 
Muuguzi Msaidizi kitengo tiba na matunzo katika hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Shinyanga, Eveline Kayanda akionesha namna wanavyopanga mafaili ya watoto.
Mtoa huduma ngazi ya Jamii/MVIU Mshauri kutoka mkoa wa Mara, Judith Bwire akionesha mpangilio mzuri wa mafaili ya wateja.
Muuguzi / Mkunga kitengo tiba na matunzo katika hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Shinyanga Grace Kali akionesha dawa za kufubaza makali ya VVU.
Eveline Kayanda akionesha kitabu cha kumbukumbu za wateja.
WAVIU Washauri wakiondoka katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga.
Kushoto ni Mratibu wa Masuala ya Watoto,Mama na Baba kutoka AGPAHI mkoa wa Shinyanga, Aminael Tesha akiwa ameongoza na washiriki wa warsha ya siku tatu ya WAVIU Washauri halmashauri sita za wilaya mkoa wa Shinyanga wakiwa katika Kituo cha Afya Cha Kambarage kilichopo katika manispaa yaShinyanga wakati wa ziara ya mafunzo kwa njia ya matembezi katika kituo hicho.
WAVIU Washauri wakiangalia mpangilio wa mafaili ya wateja katika kituo cha afya cha Kambarage.
Kulia ni Muuguzi katika kituo cha tiba na matunzo cha kituo cha afya Kambarage, Sabina Samwel akielezea utaratibu wanaoutumia kutunza kumbukumbu za wateja wanaofika katika kituo hicho.
Wa pili kulia ni Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Watu Wanaoishi na VVU katika Manispaa ya Shinyanga,Vedastus Mutangira akifafanua namna wanavyoshirikiana kufuatilia wateja wanaopotea katika huduma.

PICHA ZA MATUKIO YALIYOJIRI SIKU YA TATU YA WARSHA YA WAVIU KABLA YA WARSHA HIYO KUFUNGWA
Mratibu wa Kudhibiti Ukimwi halmashauri ya Mji Kahama, Elibariki Minja akielezea namna ya kuandaa mpango kazi kwa WAVIU Washauri.
WAVIU Washauri wakifanya kazi ya kundi kuandaa mpango kazi.
Kazi ya vikundi ikiendelea.
Mwezeshaji katika warsha hiyo, Vedastus Mutangira akiangalia kazi ya kundi.
Kazi za makundi zikiendelea.
Brown Christian kutoka halmashauri ya wilaya ya Ushetu akiwasilisha kazi ya kundi lake.

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527