MKUU WA SHULE ASIMAMISHWA KAZI KWA KUTAPELI WAZAZI WA WANAFUNZI





Mkuu wa Shule ya Sekondari Mchikichini wilayani Ilala amekamatwa na polisi akituhumiwa kushirikiana na matapeli kujipatia fedha kutoka kwa wazazi wanaohamisha watoto shule.


Ofisa Elimu Mkoa wa Dar es Salaam, Hamis Lissu amesema leo Ijumaa Februari 2,2018 kuwa mwalimu huyo alikamatwa baada ya polisi kumnasa kijana aliyekuwa akisakwa kwa utapeli na kughushi saini.

Hata hivyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Salum Hamduni alipoulizwa na mwandishi wa MCL Digital kuhusu kushikiliwa kwa mtuhumiwa huyo amesema hajapata taarifa.

"Katika uchunguzi wa awali, polisi walibaini baadhi ya nyaraka zilizoonyesha kuna ushirika kati ya kijana huyo na mkuu wa shule," amesema Lissu.

Amesema kutokana na kitendo hicho, amemsimamisha kazi mkuu huyo wa shule kupisha uchunguzi.

Lissu amesema imebainika kuna nyaraka 16 za uhamisho zenye saini ya kughushi ya ofisa elimu mkoa.

Imeelezwa watuhumiwa hudai kati ya Sh25,000 na Sh200,000 kwa ajili ya uhamisho kwenye shule kama vile Jangwani, Azania na Benjamin Mkapa zilizopo mkoani Dar es Salaam.

Inadaiwa watuhumiwa hudai malipo ya Sh100,000 kugharimia uhamisho kwa sekondari za kata.

Na Beatrice Moses, Mwananchi 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527