RAIS MAGUFULI AANZA ZIARA YA SIKU NNE MKOA WA KAGERA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 06 Novemba, 2017 ameanza ziara ya kikazi ya siku 4 katika Mkoa wa Kagera.


Akiwa njiani Kutoka Chato Mkoani Geita alikokuwa mapumzikoni kuelekea Bukoba Mjini Mhe. Rais Magufuli amezungumza na wananchi wa Muleba na Kemondo, Bukoba Vijijini na kuwahakikishia kuwa Serikali itasaini mkataba na kampuni ya kutoka Jamhuri ya Korea kati ya mwezi Desemba mwaka huu na Januari mwakani kwa ajili ya kuanza kuunda meli mpya katika ziwa Victoria itakayokuwa na uwezo wa kubeba idadi kubwa ya abiria na mzigo mkubwa zaidi ikilinganishwa na meli zilizopo


“Tunaunda meli ya kisasa itakayobeba abiria wengi na mizigo mingi, na pia tutakarabati meli zilizopo za MV Victoria na MV Butiama, tunataka pamoja na kujenga barabara, tuhakikishe kuna meli za uhakika ili muweze kusafiri na kusafirisha mazao yenu kwenda kwenye masoko” amesema Rais Magufuli.


Kuhusu ufugaji Mhe. Rais Magufuli amewaagiza viongozi wa Mkoa wa Kagera kuhakikisha mifugo yote inawekwa alama kwa mujibu wa sheria, ili kurahisisha utambuzi wa mifugo inayoingizwa nchini kutoka nchi jirani na pia kudhibiti ruzuku inayotolewa na Serikali kwa dawa za mifugo ya hapa nchini.


“Tanzania sio shamba la kuchungia mifugo ya nchi jirani, ndio maana tumeamua kukamata mifugo na kuchukua hatua kwa mujibu wa kisheria, na hata huko kwenye nchi jirani wakishika mifugo ya kutoka Tanzania wachukue hatua za kisheria za nchi hizo” amesisitiza Mhe. Rais Magufuli.


Hata hivyo amewataka wananchi wa Kagera kuacha kuvamia maeneo ya hifadhi ikiwemo hifadhi ya Burigi na ameagiza viongozi wa Wilaya ya Muleba kufuatilia madai ya wananchi juu ya kuuzwa kwa ardhi ya kijiji kulikosababisha wananchi kukosa maeneo ya kulima na kulisha mifugo yao.


“Na kuna watu waliouziwa ranchi na Serikali, watu hao hawajaziendeleza ranchi hizo na badala yake wanawakodisha wananchi, wafuatilieni na mkiona hawajaziendeleza nyang’anyeni muwape wananchi wazitumie kwa ufugaji, lakini pia hakikisheni wananchi hawavamii maeneo ya hifadhi yaliyotengwa” ameongeza Mhe. Rais Magufuli.


Aidha, Mhe. Rais Magufuli amewaagiza viongozi wa Mkoa na Wilaya za Mkoa wa Kagera kuwachukulia hatua maafisa wote wa halmashauri ambao bado wanawatoza ushuru wakulima wanaosafirisha mazao yaliyo chini ya tani moja kwa kuwa tayari Serikali imeshaamua kuondoa adha hiyo na kuwawezesha wakulima wadogo kunufaika na kilimo chao.


Mchana wa leo (06 Novemba, 2017) Mhe. Rais Magufuli atafungua mradi wa upanuzi wa uwanja wa ndege wa Bukoba.


Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Bukoba
06 Novemba, 2017

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527