KIJANA AFARIKI KATIKA AJALI MBAYA YA GARI WAKATI AKIWAHI MAHAKAMANI KUSIKILIZA HUKUMU YA MAMA YAKE


Mahakama ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Arusha/ Arumeru imewatia hatiani waliokuwa wafanyakazi 6 wa Benki ya Exim tawi la Arusha na kuwatupa jela jumla ya miaka 27. 

Watuhumiwa hao walishitakiwa kwa makosa 318, ikiwa ni pamoja na kughushi, kuharibu nyaraka, utakatishaji fedha haramu na wizi wa dola za kimarekani 521,000 mali ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA). 

Wakati hukumu inatolewa, mmoja wa waliotiwa hatiani amempoteza mtoto katika ajali ya gari, wakati kijana huyo akisafiri kuwahi kusikiliza hukumu ya mama yake. 

Kijana huyo ni mfanyakazi wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), David Chijana. 
Akisoma hukumu hiyo kwa zaidi ya saa 5 kuanzia saa 4.30 asubuhi hadi saa 9.07 alasiri, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo Deusdedit Kamugisha aliwataja aliowatia hatiani ni pamoja na mshitakiwa namba mbili Liliani Mgeye (33), Daudi Nhosha (39), Doroth Chijana (50), Genes Massawe (32), Christopher Lyimo (34) na Deusdedit Chacha (35). 

Aidha, mahakama hiyo imewaachia huru watuhumiwa saba kwa kile ilichoeleza kuwa upande wa mashitaka umeshindwa kuthibitisha makosa yao. 

Hakimu Kamugisha aliwataja walioachiwa huru na mahakama baada ya upande wa Jamhuri kushindwa kuthibitisha katika ushahidi wao kuwa watuhumiwa hao walitenda makosa hayo kuwa ni pamoja na mshitakiwa wa kwanza katika kesi hiyo ambaye alikuwa Meneja Mkuu wa Benki ya Exim (T) Ltd tawi la Arusha, Bimel Gondaili. Wengine ni pamoja na Livingstone Mwakihaba (37) maarufu kwa jina la Stone, Joyce Kimaro (36), Evance Kashebo (40), Tutufye Agrey (32), Joseph Neki(30) na mfanyabiashara Gervas Lubuva(54). 

Adhabu 
Hakimu Kamugisha alisema katika hukumu yake kwa mujibu wa sheria ya utakatishaji fedha haramu, kifungo cha chini ni miaka mitano na kuharibu nyaraka na kughushi ni miaka 14.

Hata hivyo kwa mujibu wa hukumu iliyosomwa, mtuhumiwa Mgeye, Chijana na Chacha ambao wamekutwa na makosa yote mawili, watatumikia kifungo cha miaka mitano jela bila ya faini kila mmoja. 

Aidha alisema watuhumiwa wengine waliokutwa na makosa ya kughushi nyaraka na kuharibu nyaraka ambao ni pamoja na Nhosha, Massawe na Lyimo wamehukumiwa kwenda jela miaka minne kila mmoja kwa kosa hilo. 

Awali kabla ya kusomwa kwa hukumu hiyo, Mwendesha mashitaka wa serikali, Felix Kwetukia aliitaka mahakama kutoa adhabu kali dhidi ya waliotiwa hatiani kwa kuitaka mahakama kufuata sheria ya kifungo cha miaka mitano jela ama faini ya kiwango cha chini cha shilingi milioni 100 kila mmoja. 

Kwetukia alisema serikali imeibiwa fedha za umma zilizotakiwa kufanya maendeleo kwa jamii, lakini wahusika walifanya wizi na kujitajirisha wao bila ya woga hivyo adhabu kali inahitajika. 

Kutokana na hoja hiyo mawakili wa utetezi wakiongozwa na Philipo Mushi waliiomba mahakama kutoa nafuu ya hukumu kwa waliotiwa hatiani kwani ni kosa lao la kwanza na wamejutia kosa hilo na pia wanafamilia inayowategemea. 

Ajali ya gari 
Chijana ambaye ni miongoni mwa watu wawili waliokutwa na mauti baada ya gari walilokuwa wakisafiria aina ya Toyota Mark X Saloon yenye rangi nyeusi, ikiwa na namba za usajili T796 DFG inadaiwa ndiye alikuwa dereva akitokea Moshi mkoani Kilimanjaro, kuelekea Arusha jana asubuhi. 

Imeelezwa kuwa Chijana alipata ajali katika barabara kubwa ya Moshi-Arusha, makutano ya Momella, Usa-River ambayo ni sehemu ya Wilaya ya Arumeru. 

Ilielezwa na watoa habari kuwa mmiliki wa gari hilo, David Chijana, kabla ya kupata ajali alionywa na askari wa usalama barabarani na kupigwa faini ya shilingi 30,000 kutokana na mwendo kasi na pia taa zake za breki kuwa na matatizo. 
Imeelezwa kuwa alilipa faini na kuendelea na safari kabla ya kupata ajali iliyomtoa uhai yeye na mwenzake ambaye bado kutambulika, kwa mujibu wa Polisi. 

Imeelezwa kuwa gari hilo likiwa katika mwendo kasi lilipofika katika makutano ya Momella, dereva alijaribu kupita gari lingine ndipo alipokutana uso kwa uso na basi, lililokuwa likisafiri kutoka Arusha kwenda Dar es Salaam na kujaribu kukwepa ajali. 

Kwa mujibu wa mashuhuda, Chijana alifanikiwa kulitoa gari katika hali ya kugongana uso kwa uso na basi hilo lakini gari lilimshinda likaserereka na kugonga mti mkubwa.
Kwa sababu ya spidi na kujigonga kwenye mti kwa kishindo, gari hilo lilirushwa juu na kupinduka, tairi juu na kuwaua watu wote wawili waliokuwamo humo. 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Charles Mkumbo alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kuongeza kuwa atatoa taarifa rasmi pamoja na jina la marehemu wa pili baada ya upelelezi kukamilika. 
Inadaiwa pia, mmoja kati ya waliokufa ambaye ni mfanyakazi wa TPA alikuwa anatarajia kufunga ndoa hivi karibuni. 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527