Picha : MAHAFALI YA KWANZA YA KIDATO CHA NNE 2017 KWA WAATHIRIKA WA NDOA NA MIMBA ZA UTOTONI SHULE YA AGAPE KNOWLEDGE OPEN SCHOOL


Leo Ijumaa Oktoba 20,2017 kumefanyika Mahafali ya Kwanza ya Kidato cha nne shule ya Sekondari “Agape Knowledge Open School” ambapo jumla ya watoto yatima na waathirika wa ndoa na mimba za utotoni 29 wanahitimu masomo yao kupitia mfumo wa elimu usio rasmi mwaka huu. 


Mahafali hayo yamefanyika katika shule hiyo iliyopo katika mtaa wa Busambilo kata ya Chibe manispaa ya Shinyanga na mgeni alikuwa Afisa Elimu Taaluma mkoa wa Shinyanga,James Malima kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack. 

Awali akizungumza wakati wa mahafali hayo,Mkuu wa shule hiyo ,Adili Haruni Nyaluke alisema wanafunzi hao walianza masomo yao mwaka 2014 wakiwa 54 wote wasichana na wanaohitimu ni 29. 

Naye Mkurugenzi wa shirika lisilo la kiserikali la Agape AIDS Control Programme (AACP),linalomiliki shule hiyo,John Myola alisema hayo ni ya mahafali ya kwanza kwa wanafunzi hao ambao waliokolewa katika ndoa na kurudishwa shuleni kupitia mfumo wa elimu Masafa ‘Elimu ya watu wazima’. 

“Wahitimu ni wanafunzi ambao historia yao ya elimu ilihuishwa mwaka 2014 baada ya kuokolewa katika ndoa na kurudishwa shule kupitia mfumo usio rasmi wa elimu ya watu wazima”,alieleza Myola. 

“Uwepo wa wanafunzi hawa ulisababisha shirika letu kuanzisha kituo cha elimu ya sekondari cha Agape Knowledge Open School chenye usajili namba IAE/OS/0273 ambao ulitolewa na Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima”,aliongeza Myola. 

Myola aliwataka wazazi na walezi kuwasaidia watoto hao pindi watakaporudi nyumbani kupumzika wakati wakisubiri matokeo ya na kuwakumbusha kuwa hawarudi nyumbani kuolewa. 

“Wanaporudi nyumbani siyo kwamba wanarudi kuolewa,bado hawajamaliza masomo,watoto hawa wana uwezo mkubwa darasani,tuna imani watafaulu vyema katika mtihani wao,mnachotakiwa kufanya ni kuwalea katika ustawi unaotakiwa,msiwaache peke yao,msiwaozeshe”,alisema Myola. 

Katika risala yao kwa mgeni rasmi,wahitimu hao walisema elimu waliyoipata imewapatia msingi mzuri wa kujiunga na elimu ya juu lakini pia imewajengea uwezo mzuri wa kujitambua,kufikiri,kufanya maamuzi sahihi na mambo kadha wa kadha ikiwemo elimu ya ujasiriamali,stadi za maisha na stadi za kazi na afya ya uzazi. 

Wahitimu hao pia walipaza sauti kuhusu kesi zao kuhusu vitendo vya ukatili wa kijinsia kwamba kesi zinachukua muda mrefu pasipo sababu za msingi na mwisho wake unakuwa haueleweki. 

“Tunaomba kesi za watoto zinazofikshwa katika vyombo vya sheria haki itendeke,kesi nyingi zinazohusu watoto zimekuwa zikichezewa sana na kuwa na mwisho mbaya hasa za mimba,kubakwa,vipigo,kutelekezwa ili ukweli ujulikane na haki ya mtoto ipatikane”,ilieleza sehemu ya risala yao. 

Wahitimu hao pia walitaka wazazi wanaolazimisha watoto waolewe na wanaume wanaotia mimba wapatiwe adhabu kali na wanapofikishwa mahakamani kesi zao zisichukue muda mrefu kama sheria zinavyoelekeza. 

Aidha waliyaomba mashirika mbalimbali kushirikiana na shirika la AGAPE linalomjali,kumlinda,kumthamini na kumsaidia mtoto wa kike katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia,ndoa na mimba za utotoni mkoani Shinyanga. 

Akizungumza katika mahafali hayo,Mgeni rasmi James Malima alisema serikali inatambua jitihada mbalimbali zinazofanywa na shirika la AGAPE katika kumkomboa motto wa kike kielimu na kuahidi kuwa serikali itaendelea kushirikiana nao bega kwa bega ili kuhakikisha kuwa watoto wa kike wanapata elimu. 

“Watoto wa kike wanapitia changamoto nyingi,kinachotakiwa wazazi na walezi pamoja na jamii kwa ujumla tushirikiane kuwalinda watoto wa kike na tuwapatie elimu,mtoto anapaswa kwenda shule siyo kuozeshwa”,alisema Malima. 

Hata hivyo aliwataka wazazi kuacha tabia ya kuozesha watoto kwa tamaa ya mali na wengine kuwapeleka katika nyumba za watu kufanya kazi za ndani bali wawapeleke shule ili waweze kutimiza ndoto zao. 

ANGALIA PICHA ZA MATUKIO HAPA CHINI
Wahitimu 29 wa kidato cha nne shule ya Sekondari Agape Knowledge Open School wakiingia ukumbini wakati wa mahafali ya kwanza katika shule hiyo leo Ijumaa Oktoba 20,2017- Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Maandamano kuelekea ukumbini 
Mgeni rasmi na viongozi mbalimbali wakiwa katika maandamano kuelekea ukumbini
Mgeni rasmi ,Afisa Elimu Taaluma mkoa wa Shinyanga,James Malima kwa niaba ya Mkuu wa mkoa wa Shinyanga,Zainab Telack akizungumza wakati wa mahafali ya kwanza ya kidato cha nne katika shule ya sekondari Agape Knowledge Open School
Afisa Elimu Taaluma mkoa wa Shinyanga,James Malima akizungumza katika mahafali hayo.Kushoto ni mwenyekiti wa mtaa wa Busambilo kata ya Chibe ilipo shule ya  Agape Knowledge Open School, Charles Mayunga. Kulia ni Mkurugenzi wa shirika la Agape AIDS Control Programme (AACP),linalomiliki shule hiyo,John Myola.
Wahitimu wa kidato cha nne wakiimba wakati wa mahafali hayo
Mkurugenzi wa shirika lisilo la kiserikali la Agape AIDS Control Programme (AACP),John Myola akizungumza wakati wa mahafali hayo ambapo aliwataka wazazi kuacha tabia ya kuozesha watoto kwa tamaa ya mali na badala yake wawapeleke shule
Wahitimu wakifurahia jambo wakati Mkurugenzi wa shirika lisilo la kiserikali la Agape AIDS Control Programme (AACP),John Myola akizungumza.

Mkurugenzi wa shirika lisilo la kiserikali la Agape AIDS Control Programme (AACP),John Myola akisisitiza "Mtoto wa Kike Shule"
Mwenyekiti wa mtaa wa Busambilo kata ya Chibe ilipo shule ya  Agape Knowledge Open School Charles Mayunga akilishukuru shirika hilo kwa kuwapa elimu watoto ambao wameokolewa katika ndoa
Wanafunzi wanaobaki wanaosoma katika shule ya Agape Knowledge Open School wakiimba wimbo kulishukuru shirika la AGAPE jinsi linavyosaidia watoto wa kike
Mkuu wa shule  ya sekondari Agape Knowledge Open School ,Adili Haruni Nyaluke akielezea historia ya shule hiyo
Wanawake waliopatiwa elimu ya ujasiriamali na shirika la AGAPE wakiimba na kucheza wakati wa mahafali hayo
Wazazi na walezi wakiwa katika mahafali hayo
Wahitimu wa kidato cha nne wakiwa ukumbini
Wahitimu wa kidato cha nne wakiimba na kucheza
Wahitimu wakiimba wakati wa mahafali hayo
Wageni waalikwa wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea wakati wa mahafali hayo
Wazazi na wageni waalikwa wakiwa katika eneo la tukio
Wanafunzi kutoka shule ya Sekondari Tinde wakiwa katika mahafali hayo
Mmoja wa wahitimu wa kidato cha nne katika shule hiyo akitoa ushuhuda kuhusu mimba na ndoa za utotoni wakati wa mahafali hayo
Wanafunzi wanaobaki wakicheza muziki
Wahitimu wa kidato cha nne katika shule hiyo wakisoma risala kwa mgeni rasmi
Wanafunzi wanaobaki wakisoma shairi
MC Mwamba akitoa maelekezo wakati wa mahafali hayo
Kaimu afisa elimu msingi wilaya ya Shinyanga Beatrice Mbonea akizungumza wakati wa mahafali hayo
Wageni waalikwa na wafanyakazi wa shirika la AGAPE wakiwa katika eneo la tukio
Mgeni rasmi ,Afisa Elimu Taaluma mkoa wa Shinyanga,James Malima akitoa cheti cha kufanya vizuri katika masomo kwa mmoja wa wahitimu wa kidato cha nne katika shule ya Agape Knowledge Open School. 
Mhitimu akishikana mkono na mgeni rasmi wakati akipokea cheti
Mhitimu akishikana mkono na mgeni rasmi wakati wa zoezi la ugawaji vyeti kwa wanafunzi waliofanya vizuri katika masomo yao
Zoezi la utoaji vyeti linaendelea
Zoezi la utoaji vyeti linaendelea
Wageni waalikwa wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea
Mahafali yanaendelea
Mkurugenzi wa shirika lisilo la kiserikali la Agape AIDS Control Programme (AACP),John Myola akimwongoza mgeni rasmi Afisa Elimu Taaluma mkoa wa Shinyanga,James Malima (kulia) kwenda kuangalia ujenzi wa majengo mbalimbali unaoendelea katika shule hiyo ambayo sasa ina jengo moja tu linaloonekana pichani ambalo linatumika kama darasa lakini pia kama bweni la wanafunzi.
Mkurugenzi wa shirika lisilo la kiserikali la Agape AIDS Control Programme (AACP),John Myola akielezea kuhusu ujenzi huo
Mkurugenzi wa shirika la Agape AIDS Control Programme (AACP),John Myola akielezea kuhusu ujenzi wa majengo katika shule hiyo mpya inayokabiliwa na changamoto mbalimbali kama vile upungufu wa samani,ukosefu wa umeme na maji
Afisa Elimu Taaluma mkoa wa Shinyanga,James Malima akiondoka katika eneo panapojengwa majengo mbalimbali katika shule hiyo.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527