BABA ABAKA MTOTO WAKE WA MIAKA 12 NA KUMPA MIMBA,NI BAADA YA MKEWE KUUGUA SHINYANGA


Mwanamme aitwaye Oswald Charles (40) mkazi wa mtaa wa Songambele kata ya Kitangiri mjini Shinyanga kwa anashikiliwa na jeshi la polisi mkoani Shinyanga kwa tuhuma  ya  kumbaka na kumsababishia ujauzito mtoto wake wa kambo mwenye umri wa miaka 12 (Pichani jina limehifadhiwa) ambaye mama yake ni mlemavu.

Mtuhumiwa  huyo anadaiwa kuanza kumbaka mtoto huyo tangu akiwa umri wa miaka 10 akisoma darasa la nne na hivi sasa yupo darasa la sita ambapo alipombaka kwa mara ya kwanza alimtishia kumchoma kisu iwapo angepiga kelele.

Akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake juzi kwa majonzi makubwa mama mzazi wa mtoto aliyebakwa, (33) alisema alianza kutilia shaka nyendo za mumewe kutokana na jinsi zilivyokuwa zikibadilika kila mara kuhusiana na malezi ya mtoto wake huyo.
Mama huyo alisema mashaka yalizidi pale mumeme alivyokithiri kumwonea  wivu  mwanaye kila alipokosekana nyumbani.

Mama huyo ambaye ni mlemavu aliyepooza baadhi ya viungo vyake ikiwemo macho kutokuona vizuri alisema tabia ya mumewe ilibadilika mara baada ya yeye kupatwa na maradhi aliyonayo hivi sasa na kulazimika kwenda kutibiwa kwa waganga.
Kutokana na maradhi yake, mwanaye huyo alilazimika kwenda nyumbani kwake kuishi na wadogo zake wawili ili aweze kuwahudumia kwani hapo awali.

“Tumeoana na mme huyu, mwaka 2006 baada ya kuachana na mume wangu wa kwanza niliyezaa naye watoto wawili akiwemo huyu wa kike, baada ya kuoana tumeishi vizuri na tukapata watoto wawili wa kiume, hatukuwa na tatizo mpaka pale binti yangu alipokuja kuishi hapa nyumbani nilipopata matatizo ya ugonjwa”,alieleza Mama huyo.

“Nilianza kufuatilia nyendo zake alipoanzisha tabia ya kuamka nyakati za usiku na kutoka nje na kila nikimuuliza kulikoni,anasema anafuatilia kuona nje kuna kitu gani, na hukaa huko kwa masaa kadhaa, siku moja nilikuta amesimama kwenye mlango wa binti yangu nikamuuliza kulikoni akawa mkali,” aliongeza.

Alisema  tabia ya mumewe kutoka nje usiku iliendelea na hivi karibuni aliamua kufuatilia nyendo zake na kufanikiwa kumkuta chumbani kwa binti yake akiwa amekaa kitandani na kushtushwa na hali hiyo na alipoanza kuhoji mumewe alikuwa mkali na alitishia kumpiga.

Hata hivyo alisema kulipopambazuka alianza kumhoji binti yake kwa nini baba yake aliingia chumbani kwake usiku,binti akasema baba yake alikuwa akimlazimisha kufanya naye tendo la ndoa kwa nguvu japokuwa alidai kuwa hakufanya naye jambo lolote.

“Kwa kweli nilisikitika sana kwa kitendo hicho niliamua kumweleza kaka yangu hali halisi ilivyo, lakini nilishangaa wakati namwelezea ghafla mume wangu alituvamia na kuanza kunishambulia kwa kipigo mpaka nikapoteza fahamu, na hivyo majirani walifika na kunisaidia na walipoelezwa mkasa mzima walimkamata na kumpeleka polisi,”  alieleza.

Aliendelea kueleza baada ya mtuhumiwa kupelekwa polisi majirani walimchukua binti yake na kumpeleka hospitali alikopatiwa fomu namba tatu na alipopimwa ilibainika kuwa na ujauzito wa wiki saba na siku tano na kwamba taarifa ya daktari ilieleza huko nyuma aliwahi kufanyiwa vitendo vya ukatili wa kijinsia na unajisi kwa mtoto.
Kwa upande mwingine mama huyo ametoa wito kwa wasamaria wema wenye uwezo wa kumsaidia ili aweze kutibiwa tatizo la ugonjwa unaomsumbua hivi sasa la kupooza miguu yake yote miwili na macho kupoteza uwezo wa kuona ili aweze kupatiwa matibabu na kuweza kupona ili aendelee kuwalea watoto wake ambao bado ni wadogo.


Jeshi la Polisi limethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba mtuhumiwa huyo anatarajiwa kufikishwa mahakamani kujibu shtaka la ubakaji baada ya kukamilika kwa upelelezi wa kina. 

Na Kadama Malunde-Shinyanga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527