KUHUSU WAMASAI WAISHIO UWANJA WA NDEGE WA KIA KUMGOMEA WAZIRI PROFESA TIBAIJUKA



Viongozi wa kimila wa kabila la wamasai waishio katika vijiji vitano vinavyozunguka uwanja wa ndege wa kimatifa (KIA)wamepinga agizo la waziri wa nyumba, ardhi na makazi Prof. Anna Tibaijuka la kuwataka waondoke katika maeneo yao kwa ajili ya kupisha upanuzi wa uwanja bila kuwasikiliza.

Wakizungumza kwenye kikao cha kujadili mgogoro huo viongozi hao wamemtaka waziri Tibaijuka kufika katika vijiji hivyo na kuwasikiliza wananchi badala ya kutoa maagizo ya kuhamishwa akiwa ofisini kwa kuwa mgogoro huo tayari wameufikisha katika ofisi ya waziri mkuu na kwamba wanasubiri majibu ya tume iliyoundwa.

Wamesema hawako tayari kuondoka katika maeneo hayo ambayo uwanja uliwakuta na kwamba tayari wameshajiimarisha na kuweka miundombinu ya zahanati shule, afya, maeneo ya kilimo na malisho ya mifugo.


Kwa upande wake diwani wa kata ya KIA Mh.Sinyork Ole Nanyoki amesema wananchi wa vijiji hivyo wana hati miliki ya maeneo yao licha ya serikali kutoa hati miliki bandia kwa uongozi wa kiwanja cha ndege, na kwamba ni vema viongozi wa serikali wakatumia busara kutatua mgogoro huo ambao unaweza kuhatarisha amani.

Akizungumza na watendaji wa idara ya ardhi katika ofisi ya mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro waziri wa nyumba ardhi na makazi Prof Anna Tibaijuka alisema haoni sababu ya wananchi kuendela kuishi katika maeno hayo badala yake wapewe fidia ili kupisha uwanja wa ndege.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527