
Brigedia Jenerali, Kongo Zoma amesema Jeshi la Wananchi Tanzania
(JWTZ) linahitaji wasomi wanaoendana na teknolojia iliyopo na wala
halina nafasi kwa waliofeli.
Brigedia Zoma alisema hayo jijini Dar es salaam jana katika mahafali ya 19 ya kidato cha nne katika Shule ya Sekondari ya Airwing.
“Jeshini tunahitaji watu waliobobea katika elimu
kwa kuwa tunatumia sayansi ya hali ya juu. Tunahitaji wasomi wenye
uelewa wa kutosha na siyo mapooza,” alisema Brigedia Zoma.
Aliwataka wanafunzi hao kuzingatia elimu kwa kuwa ndiyo ufunguo na msingi wa maisha yao ya baadaye.
Pia aliwataka wazazi na walezi kuwekeza elimu kwa watoto wao ambayo ndiyo utajiri pekee usiofilisika.
Brigedia Zoma aliwataka wanafunzi kuwa makini na
matumizi ya simu za mkononi kwa kuwa zinaweza kuharibu mfumo mzima wa
malengo yao.
“Hakikisheni mnakuwa makini na simu za mkononi,
mjihadhari na mjiepushe na vitendo vya uhalifu na matumizi ya dawa za
kulevya, zingatiemi sana maadili mliyopewa na mjiendeleze zaidi
kielimu... msikubali kuishia hapa mlipo,” alisema.
“Taifa bila elimu ni sawa na upuuzi mtupu, hivyo tunahitaji viongozi wenye elimu wanaojua kuchanganua mambo na siyo wapuuzi.”
Kwa upande wa wahitimu hao, waliahidi kufanya vizuri katika mtihani wa taifa wa kumaliza kidato cha nne.
Pia walisema wazazi na walezi wanapaswa kuwalipia ada kwa wakati watoto wao ili wasome kwa amani.
via>>Mwananchi
via>>Mwananchi
Social Plugin