MADIWANI WA CHADEMA SHINYANGA WALIOJIUZULU NA KUHAMIA CCM WAMEVURUGWA,SASA KUHAMIA TENA CHADEMA

Habari zilizoufikia mtandao huu wa malunde1 blog ni kwamba wale madiwani wa chadema Sebastian Peter na Zacharia Mfuko katika manispaa ya Shinyanga waliojiuzulu mwanzoni mwa mwaka huu na kujiunga rasmi na CCM, sasa hali ni tete,inadaiwa kuwa leo watatangaza uamuzi mgumu wa kuhamia tena CHADEMA katika mkutano wa hadhara eneo la viwanja vya Mahakama ya Mwanzo Nguzo nane.

Sebastian Peter na Zacharia Mfuko wakihamia ccm walidiriki kuchoma hadi nguo za Chadema hadharani


"KAMA KWELI WATARUDI CHADEMA,JE KIPI CHAMA SAHIHI,CHADEMA AU CCM?,NA JE NAPE WA CCM ALIYEWANYAKUA MADIWANI HAO ATAFICHA WAPI SURA YAKE!!,NA JE?DR SLAA ALIYEKITUHUMU CCM KWA SIASA CHAFU BAADA YA KUDAI MADIWANI HAO KUHONGWA NA CCM NAYE ANAWAZA NINI?,MACHO NA MASIKIO LEO MJINI SHINYANGA KUANZIA SAA SABA MCHANA,NA JE WANACHAMA WA CCM NA CHADEMA WANACHUKULIAJE SAKATA HILI,AIBU YA NANI HII AU NDIYO SIASA YENYEWE "
Malunde1 blog itakuwepo eneo la tukio>>>Endelea kutembelea blog hii

Mtandao huu umepata taarifa ifuatayo kupitia Jamii Forums,shuka nayo uone mambo
Madiwani waliohama chadema shinyanga kwa hila za MM na Nape waeleza vyanzo vya mapato ya ACT, waomba radhi warejeshwe chadema


Madiwani wawili waliohamia CCM kutoka CHADEMA, katika kata za Ngokolo na Masekelo, Shinyanga, Sebastian Peter na Zacharia Mfuko, wameibuka na kusema wanajutia uamuzi wao, na sasa wanafanya jitihada za kuomba warejeshewe uanachama wa CHADEMA baada ya kukerwa na hila za CCM na ACT.



Madiwani hao wanadai kuwa walihamia CCM kwa muda -kwani waliambiwa kuwa ACT kitakapokuwa kimepata usajili wa kudumu wangejiunga nacho ili kuimarisha upinzani nchini.

Madiwani hao walijiunga na CCM Februari mwaka huu na kupokelewa na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nauye. Baadaye, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk Wilbroad Slaa alikituhumu CCM kwa mchezo mchafu.

“Tulishawishiwa kuhamia CCM kwa muda kwa lengo la kuhamia ACT ili kikipata usajili wa kudumu tuhamie huko pamoja na baadhi ya wanachama wa CCM.

“Tuliambiwa tufanye siasa za harakati, lakini tulichobaini ni kuwa tangu tukubali mawazo hayo ya viongozi wa ACT tukijua tunaimarisha upinzani imekuwa tofauti. Mkakati huo ulianza kuratibiwa na Mwenyekiti wa UVCCM, Abbakari Gulam ambaye ni mtoto wa Meya wa Shinyanga, wakiwa na Habib Mchange, kisha tuliona mkakati unatekelezwa na mbunge wa Shinyanga mjini, Stephen Masele, Nape Nauye, Januari Makamba, Mwigulu Nchemba na Ridhiwani Kikwete,” walisema katika taarifa yao mbele ya waandishi wa habari jijini Mwanza.

Wakisimulia mkakati huo walisema walifikishwa Tinde na kiongozi huyo wa UVCCM kisha wakiwa huko walipigiwa simu na Stephen Masele na kuzungumza Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA aliyewahakikishia kuwa baada ya kuondoka CHADEMA watajiunga na ACT ili iwawezeshe kupata nafasi za uongozi wa kitaifa katika chama hicho kipya, pamoja na kupatiwa kitita kikubwa cha fedha.

Chanzo chetu cha habari kutoka Shinyanga kimeelezwa kuwa baada ya kuhamia walipatiwa kiasi kikubwa cha pesa bandia, na katika kitita hicho waliambulia laki mbili ndio zilikuwa halali, pesa hizo zimetajwa kuwa zilikuwa ziwe milioni kumi na mbili lakini bada ya kuhesabu zilipatikana halali laki mbili tu, na zinadaiwa kutolewana na msaidizi wa Masele akiwa na Mchange katika hoteli ya Karena iliyopo Shinyanga, kabla ya madiwani hao kuondolewa na gari hadi Mwanza na kusafiri kwa ndege hadi Dar es Salaam kwa maelekezo ya Nape.

Tamko hilo linaongeza kuwa “kwa kipindi chote cha kudanganywa tulidhani Zitto anaonewa, hivyo tukaamua kujiunga na Chama chake ambacho alituhakikishia lakini tumebani kuwa ACT na CCM hawana tofauti, mikakati inatengenezwa na ACT ila watekelezaji ni CCM, baada ya kubaini ghiliba hizi tumeshindwa tumetafakari kuwa hata barua zetu tuliandika zikiwa na makosa ya kikanuni hivyo sasa tumemwandikia tena Meya kumuuliza ni kwanini hajatualika kwenye vikao viwili kwa kuwa tulikuwa hatujajiuzulu kisheria.

“Ili mtu kujiuzulu udiwani, kanuni zinasema kuwa diwani anaandika barua kwa Meya, unaambatanisha na kitambulisho cha udiwani, na hati ya ushindi ya udiwani ambayo hatujawapa wala vitambulisho vyetu, tulichokifanya ni kama kuandikiana barua za kawaida tu, na mtu kutangaza kujiunga na Chama kiingine bila kuchukua kadi yao sisi sio wanachama wao na kwa kuwa Chama chetu hakijachukua hatua zozote dhidi yetu basi tunarejea kwetu upinzani kushindana na CCM,” alisema Sebastian mbele ya waandishi wa habari.

Walisema CCM na ACT waendelee na kamari zao kuhadaa watanzania, “jamaa hao wana umakini kidogo ndio maana hawakubaliani kuwa bado hatujajiuzulu kisheria wakakimbilia kutupeleka jukwaani kushangilia, sasa sisi tunarudi kutumikia wananchi wetu kwani hatujavunja sheria, hatukukiuka kanuni za kujiuzulu furaha ya CCM na ACT ni ya muda tu, tulionda huko tumewabaini.

Kufuatia hali hiyo,madiwani hao waliandika kuwa “tunapenda kuomba radhi viongozi wote wa CHADEMA, wanachama na watanzania wote watusamehe, watupokee tukapambane kufanya kazi ya siasa za upinzani wa kweli kuleta ukombozi wa kweli kwa nchi yetu, tulichokiona huku tumekijua, tunawatahahadharisha wengine wakionga inafaa wajiunge huko kwa hasara yao ya maisha yao kisiasa na kufanya kazi ya kujenga CCM.”

Mkakati huu unaratibiwa na mmoja wa wabunge wa upinzani mwenye mahusiano ya karibu na viongozi wa CCM na serikali anayedaiwa hadi sasa kuifadhili ACT mabilioni ya shilingi kwa ajili ya kujiimarisha mikoani kabla ya uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu.. 


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527