MKUU WA MKOA AAGIZA BIASHARA YA POMBE IFUNGWE

Mkuu wa Mkoa wa Magharibi Unguja, Ayoub Muhammed Mahmoud ameziagiza Manispaa za mkoa huo kusitisha leseni ya biashara za vileo katika kipindi chote cha mwezi mtukufu wa Ramadhani ambao waumini wa dini ya kiislamu duniani wameanza kufunga leo.

Akitoa tararifa kwa waandishi wa habari Mh. Mahmoud amesema hatua hiyo imelenga kuimarisha imani za watu kwa wanaofunga huku akizitaka manispaa ndani ya Mkoa huo kusimamia agizo hilo.

"Ili waumini waweze kuukabili mwenzi huu kiukamilifu ni lazima kwa wananchi kutumia fursa za ramadhani kwa kufanya mambo mema ili Mwenyezi Mungu aweze kuzikubali swaumu", amesema Mahmoud.

Aidha, Mahmoud amewataka watembezaji watalii kutoa mwongozo kwa wageni kwa kufuata utaratibu ulio sahihi kwa kuvaa mavazi ya heshima na yanayo kubalika kutokana na mila, silka na utamaduni.

Kwa upande mwingine, Mkuu wa Mkoa huyo ameliagiza Jeshi la Polisi kuongeza doria wakati wa jioni ili kuimarisha hali ya ulinzi na usalama wa raia na mali zao sambamba na kuimarisha usalama wa barabarani ili kuepusha ajali zisizo za lazima.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527