MISS TANZANIA MPYA YAZALIWA 'WAZIRI MWAKYEMBE AELEZA ALIVYOKWAZWA NA UHUNI WA LUNDENGA'

Waziri wa Habari, Utamaduni, sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe ameweka wazi kwamba alikuwa tayari kuchukua mashindano ya Miss Tanzania kutoka kwa muandaaji Hashim Lundenga kwa madai kuwa kulikuwa na uhuni ulioanza kuigubika tasnia hiyo.


Akizungumza kwenye hafla ya uzinduzi wa Miss Tanzania Mpya chini ya Mkurugenzi wa The Look Company, Miss Tanzania 1998 Bi. Basila Mwanukuzi, Dk Mwakyembe amesema kuwa uhuni wa waandaji ulishamkwaza hivyo kwa kuwa mabadiliko yameangukia mikononi mwa Basila basi anaamini 'upele umepata mkunaji'.


Akizungumzia chanzo cha kutaka kuyaweka mashindano hayo kuwa chini yake kutoka kwenye kampuni ya Lino Agency, Waziri Mwakyembe amesema kwamba alikasirishwa na uhuni aliofanyiwa Miss Tanzania 2016 kwa kupewa zawadi ya gari hewa huku akiongeza kuwa mabinti wanajitoa kwa juhudi licha ya kuwepo kwa mfumo dume kwenye jamii.


"Watotot wa watu wanajitolea, mfumo wetu bado ni dume wanapata tabu sana kuishawishi jamii kuwa haya ni mashindano ya kawaida anapita kwenye chujio anashinda alafu unampa zawadi hewa. Basila mwenyewe aliwahi kupewa zawadi hewa kaeni naye vizuri atawaeleza. hivyo niseme mabadiliko haya yamenifanya nione kwamba upele umepata mkunaji" Mwakyembe.


Hata hivyo Waziri huyo mwenye dhamana ya sanaa amemtaka muandaaji huyo mpya (Basila Mwanukuzi) kuhakikisha anaondoa ubabaishaji wote uliokuwepo na kumuahidi kuwa serikali ipo nyuma yake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527