UVCCM KIGOMA WATAKIWA KUACHANA NA SIASA ZA MANENO

Vijana wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi UVCCM mkoa wa Kigoma umetakiwa kuachana na siasa za maneno na kufanya siasa za uchumi ili kuunga mkono kauli mbiu ya rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli  ya kuanzisha viwanda.

Wito huo ulitolewa jana na mjumbe wa Halmashauri kuu ya taifa MNEC, Kilumbe Ngenda aliyekuwa mgeni rasmi katika Baraza la Vijana wa UVCCM Mkoa wa Kigoma katika uchaguzi wa wajumbe watatu wa kamati ya utekelezaji ya UVCCM mkoa na kumthibitisha katibu wa uhamasishaji na chipukizi.

Aliwataka vijana hao kubuni miradi na kuendeleza miradi waliyonayo kama jumuiya zingine zinavyofanya.

Alisema Vijana wanatakiwa kuwa na miradi yao binafsi ili kupunguza tabia ya kutembea na mabakuli kuomba na kuahidi kutoa mifuko 50 ya saruji ili kubuni mradi ikiwa ni pamoja na kuanzisha viwanda pamoja na kuiboresha nyumba ya wageni ya vijana iliyopo Manispaa ya Kigoma Ujiji ili kuinua uchumi wa vijana.

Aidha mbunge kupitia Vijana Mkoani Kigoma, Zainabu Katimba, alisema yeye kama Kiongozi wa vijana ameamua kutoa kiasi cha shilingi milioni saba kwa ajili ya kuwasaidia vijana wilaya zote kuanzisha miradi pamoja na kuanzisha viwanda na kutoa Vyerehani vitatu katika kikundi cha vijana wajasiriamali wa  kikundi cha Mwandiga.

Alisema wanaendelea na jitihada za kuhakikisha vijana wote wanakuwa na shughuli za kufanya na kila wilaya watatakiwa kubuni miradi na wao kama viongozi watahakikisha wanasaidia kuwawezesha ili kuanzisha vikundi vya ujasiriamali pamoja na kuanzisha viwanda ili kuwajengea ajira vijana.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa wa Kigoma, Silvia Sigura alisema wao kama vijana wamejipanga kufanya siasa za uchumi na siyo siasa za maneno na kwa kudhihirisha hilo wameanzisha harambee kwa vijana katika baraza lililofanyika na kufanikiwa kuchangisha mifuko 130 kwa ajili ya kuanza kujenga vibanda 12 katika kiwanja chao.

Alisema kwa michango waliyoipata watahakikisha wanaanzisha miradi kwa kila wilaya na kutoa elimu ya ujasiriamali kwa vijana ili waweze kujiajili katika masuala ya ujasiriamali na kuwawezesha vijana kuanzisha viwanda na kujiinua kiuchumi.

Na Rhoda Ezekiel - Malunde1 blog Kigoma
Mbunge wa viti maalumu kupitia UVCCM Mkoa wa Kigoma Zainabu Katimba akigawa cherehani kwa wanakikundi wa kikundi cha ujasiriamali cha vijana




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527