RAIS MAGUFULI AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA WAZIRI WA ULINZI WA ISRAEL IKULU

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli tarehe 22 Machi, 2018 amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Ulinzi wa Israel Mhe. Avigdor Lieberman Ikulu Jijini Dar es Salaam.


Mazungumzo hayo yamehudhuriwa na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dkt. Hussein Ali Mwinyi, Balozi wa Israel hapa nchini Mhe. Noah Gal Gendler, viongozi wakuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na Jeshi la Polisi.


Katika mazungumzo hayo Mhe. Rais Magufuli amemshukuru Mhe. Lieberman kwa kuitembelea Tanzania na amemhakikishia kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ina dhamira ya dhati ya kuukuza zaidi na kuuimarisha uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na Israel.


Mhe. Rais Magufuli ametaka makubaliano ya ushirikiano kati ya Tanzania na Israel katika maeneo mbalimbali yakiwemo ulinzi na usalama, mafunzo na masuala ya kiuchumi yatiwe saini haraka ili utekelezaji uanze mara moja.


“Tanzania na Israel ni marafiki wa miaka mingi, nataka kuona urafiki wetu unakuwa zaidi, nawakaribisha wawekezaji kutoka Israel kuja kuwekeza katika kilimo, madini na gesi na pia kuwepo ndege za moja kwa moja kutoka Israel hadi Dar es Salaam na Kilimanjaro ili kukuza utalii” amesema Mhe. Rais Magufuli.


Aidha, Mhe. Rais Magufuli amemuomba Mhe. Lieberman kumfikishia ujumbe Waziri Mkuu wa Israel Mhe. Benjamin Netanyahu wa kumualika kutembelea Tanzania na pia kuanzisha ofisi ya ubalozi hapa nchini badala ya kutumia ofisi za ubalozi zilizopo Nairobi nchini Kenya.


Kwa upande wake Mhe. Avigdor Lieberman amemshukuru Mhe. Rais Magufuli kwa kumkaribisha na kufanya nae mazungumzo na pia amemhakikishia kuwa Israel imejipanga kuongeza uhusiano na ushirikiano wake na Tanzania katika maeneo yote ya makubaliano pamoja na kusaidia kilimo na usindikaji wa chakula.


Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
22 Machi, 2018

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527