MWENYEKITI UVCCM KIGOMA ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI KIFO CHA DKT. KABOUROU


Mwenyekiti wa UVCCM  mkoa wa Kigoma Sylivia Sigula


Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoani Kigoma umepokea kwa masikitiko na huzuni taarifa za kifo cha aliyekuwa Mwenyekiti Mstaafu wa CCM Mkoa Kigoma Dkt. Walid Amani Kabourou aliyefariki  jana /usiku wa kuamkia leo Jumatano,Machi 7,2018 katika hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es salaam. 

Katika salamu za rambirambi kutoka kwa  Mwenyekiti wa UVCCM Mkoa Kigoma Sylivia Sigula kwenda kwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa Kigoma Ammandus Nzamba , UVCCM wameelezea kusikitishwa kwao na kifo cha kiongozi huyo mkoani humo. 

Sylivia amemuomba Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Kigoma awafikishie salamu zao za zarambirambi na mkono wa pole kwa familia ya marehemu, ndugu na jamaa na kuwataka wawe na moyo wa subira na ustahamilivu katika kipindi hiki kigumu.

Aidha Mwenyekiti huyo wa UVCCM amemtaja marehemu Dk Kabourou katika maisha yake amekuwa kiongozi aliyetawaliwa na busara, hekima, maarifa mapana na mwenye upeo mkubwa katika medani za siasa na historia ambapo mara zote amekuwa zaidi ya mwalimu kwa vijana.

"Chama chetu kimepoteza kiongozi wake bora, msikivu na mjuzi katika masuala ya siasa na maendeleo ya demokrasia .Tunamuomba mungu mtukufu ampokee, amsaheme dhambi zake na amuweka mahali pema peponi",ameeleza Sylivia katika salamu zake za rambirambi.

Hata hivyo Mwenyekiti huyo wa UVCCM amesema jumuia yake mkoani humo itaendelea kujifunza na kuyaenzi mambo yote mema na mazuri yaliyokuwa yakifanywa na Dkt. Kabourou wakati wa uhai wake na jinsi alivyokuwa mahiri katika kujenga hoja na kujibu mapigo ya kisiasa. 

Pamoja na salamu hizo za rambirambi, Sylivia amesema mwili wa marehemu Dr. Walid Kabourou utasafirishwa kutoka Dar es salaam kuelekea Kigoma Kesho saa nne asubuhi. 

Mazishi yanatarajiwa kufanyika siku ya Ijumaa,tarehe 9 Machi 2018 katika  makaburi ya Kipampa shule ya Ujiji. 

Msiba upo nyumbani kwa marehemu huko Bagwe, Kigoma Mjini

Inna lilahi wa Inna Ileiyhi Rajiun .

Imetolewa na:

Mwenyekiti wa UVCCM  mkoa wa Kigoma Sylivia Sigula

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527