DC MATIRO AFUNGUA KIKAO CHA UELIMISHAJI KUHUSU MPANGO WA ANWANI ZA MAKAZI NA POSTIKODI SHINYANGA

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro amefungua kikao  cha uelimishaji kuhusu Mpango wa Anwani za Makazi na Postikodi  kwa ajili ya kuwajengea uelewa na uwezo viongozi na watendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga ili waweze kutekeleza mpango huo ipasavyo kwa kushirikisha wadau mbalimbali.

Kikao hicho kinachoendeshwa na Wataalam wa Kamati ya Kitaifa ya Anwani za Makazi na Postikodi kimefanyika leo Jumanne Machi 6,2018 katika ukumbi wa Lewis Kalinjuna uliopo katika ofisi za Manispaa ya Shinyanga.

Matiro alisema mfumo huo utaiwezesha serikali kuwahudumia wananchi wake kwa urahisi ikiwa ni pamoja na kutoa ulinzi, kurahisisha mawasiliano miongoni mwa wananchi na serikali au sehemu za huduma na kuongeza ufanisi katika utoaji huduma za kijamii.

Aliongeza kuwa pia mfumo huo unaongeza ufanisi katika huduma za kibiashara, huduma za dharura na uokoaji, kurahisisha sensa, kuboresha huduma za Posta na kuwezesha utoaji wa biashara mtandao pamoja na kurahisisha ukusanyaji wa mapato mbalimbali ya serikali.

“Niishukuru Kamati ya Kitaifa ya Anwani za Makazi na Postikodi kwa kuichagua Manispaa ya Shinyanga kuwa miongoni mwa Halmashauri zitakazopewa elimu kuhusu mpango huu, serikali ya wilaya iko tayari kutoa ushirikiano ili sote kwa pamoja tutimize wajibu wetu katika kuifanya Manispaa ya Shinyanga kuwa ya kisasa”,alisema Matiro. 

“Serikali inasisitiza kuwa ni vyema taasisi zote za umma na zile za binafsi zianze kutumia Anwani za Makazi na Postikodi ili kuchochea kasi ya maendeleo ya nchi, na kwa kuwa Postikodi za nchi nzima zimeandaliwa ikiwemo Mkoa wa Shinyanga,Hivyo naielekeza Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kutenga bajeti kwa ajili ya uwekaji wa muundo mbinu wa Anwani za Makazi na Postikodi”,aliongeza Matiro.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Posta kutoka Wizara ya Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Caroline Kanuti alisema mpango huo ni utekelezaji wa sera ya taifa ya posta ya mwaka 2013 inayoelekeza kuwepo kwa anwani za kitaifa zitakazowezesha ufikishaji wa huduma mbalimbali za kijamii na za kibiashara kwa wananchi.

Alisema mpango huo wa mfumo wa Anwani za Makazi na Postikodi unalenga kutoa anwani ya uhakika kwa kila nyumba na sehemu za biashara na kwamba anwani hizo zitatumiwa na serikali,wananchi na wadau mbalimbali.

Aliongeza kuwa mpango huo unaendelea kutekelezwa katika mkoa wa Arusha,Dodoma na Dar es salaam huku akizitaja baadhi ya changamoto wanazokutana nazo kuwa ni ujenzi holela na mipango mji dhaifu.

Aidha Kanuti aliwataka wadau kushirikiana na kutenga fedha ya utekelezaji wa mpango huo wenye manufaa makubwa kwa maendeleo. 

ANGALIA PICHA ZA MATUKIO HAPA CHINI
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akifungua kikao  cha uelimishaji kuhusu Mpango wa Anwani za Makazi na Postikodi  kwa ajili ya kuwajengea uelewa na uwezo viongozi na watendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga- Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza wakati wa kikao hicho.Kushoto ni Mwenyekiti wa Kikosi Kazi cha Kuratibu Mpango wa Anwani za Makazi na Postikodi,Mathias Nkonya. Kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa Shinyanga Magedi Magezi.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza wakati wa kikao hicho kilichohudhuriwa pia na  Wakuu wa Idara,Wataalam wa Kamati ya Anwani za Makazi na Postikodi Manispaa ya Shinyanga,baadhi maafisa watendaji wa kata na wenyeviti wa serikali za mitaa.
Viongozi wakimsikiliza Mkuu wa wilaya ya Shianyanga Josephine Matiro.
Washiriki wa kikao hicho wakiwa ukumbini
Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Posta kutoka Wizara ya Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Caroline Kanuti akitoa elimu kuhusu Mpango wa Anwani za Makazi na Postikodi. 
Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Posta kutoka Wizara ya Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Caroline Kanuti akiendelea kutoa elimu kwa washiriki wa kikao hicho.
Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Posta kutoka Wizara ya Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Caroline Kanuti akimalizia kutoa elimu na kuwaomba washiriki wa kikao hicho kuwa mabalozi na kuifanya manispaa ya Shinyanga kuwa ya mfano 
Mkurugenzi Msaidizi Huduma za Posta kutoka Wizara ya Ujenzi,Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Caroline Kanuti akimweleza jambo Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akisalimiana  na Mwenyekiti wa Kikosi Kazi cha Kuratibu Mpango wa Anwani za Makazi na Postikodi, Mathias Nkonya (kushoto).
Picha ya pamoja: Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro na wataamu kutoka Kikosi Kazi cha Kuratibu Mpango wa Anwani za Makazi na Postikodi. Picha zote na Kadama Malunde - Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527