WANACHAMA SABA WA CHADEMA WAACHIWA HURU TUHUMA ZA KUFANYA VURUGU DAR


Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewaachia huru wanachama wa Chadema baada ya upande wa mashtaka kushindwa kuthibitisha mashtaka yao pasipo kuacha shaka.


Washtakiwa walioachiwa huru na Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba leo Jumatano Februari 28, 2018 ni; Sunday Urio, Kizito Damia, Joseph Samky, Chrisant Clemence, Wilfred Ngowi, Karim Ally na Kinyaiya Siriri.


Kwa pamoja walikuwa wanakabiliwa na tuhuma za kufanya fujo na kuwazuia askari polisi kufanya kazi yao.


Akisoma hukumu hiyo leo, hakimu Simba amesema wajibu wa kuthibitisha mashtaka pasipo kuacha shaka ni wa upande wa mashtaka na siyo upande wa utetezi .


Akiendelea kusoma hukumu hiyo amesema katika ushahidi uliotolewa na mashahidi watatu wa upande wa mashtaka, hakuna sehemu walisema, waliwaona washtakiwa wakirusha mawe kwa polisi na kuwazua wasifanye kazi yao.


Katika kesi hiyo washtakiwa walionekana na kesi ya kujibu na katika utetezi wao karibia wote ulikuwa unafanana kuwa hawakuwepo eneo la tukio na wala hawakutenda kosa waliloshtakiwa nalo.


Hivyo aliwaachia huru washtakiwa hao. Katika kesi hiyo wanadaiwa, Januari 26, mwaka 2015 huko Ubungo eneo la Riverside, kwa makusudi walifanya fujo kwa kuwarushia mawe askari polisi wa kutunza amani ili washindwe kufanya kazi yao.

Na Tausi Ally, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527