MVUA YAZUA BALAA DODOMA...WATU SABA WAHOFIWA KUFA



Watu saba wanahofiwa kufa maji kufuatia mvua kubwa zilizonyesha jana Alhamisi mkoani Dodoma.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Binilith Mahenge amesema watu hao wamekufa baada ya kuzama katika mashimo ya machimbo, makaro ya vyoo na wengine wawili hawajulikani waliko baada ya kusombwa na maji wakiwa kwenye gari eneo la Kikomho Manispaa ya Dodoma.


"Taarifa zote kamanda wetu wa polisi atawaambia lakini ni kweli Kongwa kuna watu wawili wamekufa baada ya kutumbukia kwenye shimo la choo wakiwa msibani ambapo mvua zilinyesha na kulivunja shimo hilo wakatumbukia watu sita wawili walikufa," amesema Mahenge.


Wengine ni Ramadhani Haruni mtu mzima aliyekufa ndani ya shimo la machimbo ya dhahabu Nzuguni na Daudi Luwinga (16) mkazi wa Nzuguni pia ambaye alitumbukia kwenye shimo la kujenga choo wakati akitoka kwenye mchezo wa mpira.


Katika kijiji cha Kikombo gari Toyota Mitsubishi lilisombwa na maji usiku wa kuamkia leo Ijumaa ambapo lilikuwa na dereva na abiria mmoja na wote hawajapatikana.





Dk Mahenge ambaye alitembelea maeneo yote kujionea mazingira ya ajali, amesema licha ya wingi wa mvua lakini uharibifu wa mazingira umechangia na kuwataka wakazi wa Dodoma kupanda miti kwa wingi.


Pia amepiga marufuku machimbo ya dhahabu Nzuguni na kutaka wakazi wa eneo hilo kuhama haraka na mashimo yafukiwe.


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto amesema jeshi hilo litatumia nguvu kuwaondoa watu wanaoendeleza uchimbaji wa dhahabu Nzuguni.


Muroto amesema baadhi ya watu katika eneo hilo walishalipwa fidia ambapo Serikali ililipa Sh 441.3 milioni kwa ajili ya kupisha eneo hilo ambalo limetengwa kwa matumizi ya polisi lakini bado wanaishi.


Meneja wa Tanrods Mkoa wa Dodoma, Leonard Chimagu amesema Serikali haina bajeti ya kujenga madaraja yaliyobomoka lakini watafanya kila namna ikiwemo kupanga mawe kwa lengo la kuruhusu magari kupita kwa dharura.

Na Habel Chidawali, Mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527