MWENYEKITI WA UVCCM MBARONI KWA TUHUMA ZA RUSHWA


Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Dodoma inamshikilia Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Sadifa Juma Khamis kwa tuhuma za kugawa rushwa kwa wajumbe wa mkutano mkuu wa uchaguzi.
UVCCM leo Jumapili Desemba 10,2017 inachagua viongozi wapya wa ngazi ya Taifa watakaoongoza jumuiya hiyo ya CCM kwa kipindi cha miaka mitano.
Sadifa ambaye pia ni mbunge wa Donge, Zanzibar amekamatwa nyumbani kwake karibu na mnada wa zamani mkoani Dodoma.
Kamanda wa Takukuru mkoani Dodoma, Emma Kihanga amethibitisha kukamatwa kwa mwenyekiti huyo na kwamba watatoa taarifa zaidi baadaye.
"Ni kweli tumemkamata tangu jana usiku tumekesha tunafanya uchunguzi, nitatoa taarifa baadaye kuhusu tukio hilo," amesema.
Mkutano mkuu wa uchaguzi wa UVCCM unaendelea mjini Dodoma na miongoni mwa waliohudhuria ni Mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli.
Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan akifunga mkutano mkuu wa uchaguzi wa Umoja wa Wanawake (UWT) jana Jumamosi Desemba 9,2017 alisema hawajapokea malalamiko mengi kutoka umoja huo na kuzitaka jumuiya nyingine za CCM kujifunza UWT.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527