TUNDU LISSU : KAMA WAKENYA MNGEMCHAGUA ODINGA MNGEKOMA

Rais wa TLS na Mwanasheria Mkuu wa CHADEMA, Tundu Lissu amefunguka na kusema wao kama CHADEMA waliwaambia watu wa Kenya kuwa kama watarogwa na kumchagua Raila Odinga kuwa Rais wa nchi hiyo wangekoma kwani aliweka wazi ataongoza kama Rais wa Tanzania.


Tundu Lissu anasema kuwa katika uchaguzi uliofanyika nchini Kenya tarehe 8 Agosti 2017 unatoa mafunzo mengi kwa Tanzania kwani Kenya wameweza kupiga hatua kubwa na kutoa haki ya msingi ya kupiga kura kwa wafungwa na Raia wake waliopo nje ya Kenya jambo ambalo Tanzania ni kitu kisichowezekana.


"Kenya inatufundisha umuhimu wa kuwa na Katiba mpya, Katiba ya Kidemokrasia, Katiba inayoweka uhuru kwa wale wanaoshiriki uchaguzi kwa kuweka utaratibu wa kuhakiki taratibu za uchaguzi katika kila hatua na hilo ni jambo muhimu sana, lakini Kenya inatufundisha umuhimu wa kuwa na Demokrasia tumeona wafungwa wakipiga kura, tumeona waandishi wa habari wakiruhusiwa kuiingia gerezani kueleza umma jinsi zoezi la upigaji kura linavyoendelea hata kwa watu ambao wamepata adhabu kwa mujibu wa sheria za Kenya lakini kwetu sisi hicho kitu hakipo kabisa, tumeona raia wanaokaa nje ya Kenya wameshiriki uchaguzi sisi hilo haliwezekani" alisema Tundu Lissu


Aidha Tundu Lissu amesema kwa mambo yote ambayo yameendelea Kenya katika uchaguzi yanatoa funzo kuwa na mfumo wa Demokrasia lakini pia amegusia chama cha CHADEMA kuwa rafiki na Chama Cha Jubilee na kusema siyo dhambi.


"Sisi kuwa na chama rafiki Kenya wala siyo kitu cha ajabu sana, tuna chama rafiki Ghana tunavyama rafiki kila mahali na wakati wa uchaguzi marafiki wanaungana mkono, wakati wa uchaguzi ANC wanaunga mkono CCM, Museven na NRM yake wanaunga mkono CCM na sisi kwenye uchaguzi huo wa Kenya tumeunga mkono Jubilee, na kwenye uchaguzi huu wa juzi Raila Odinga aliwaambia waKenya kuwa wakimchagua ataongoza nchi kama Rais wa Tanzania ilibidi tuwaambie Wakenya kuwa mtakoma" alisisitiza Tundu Lissu


Katika Uchaguzi uliofanyika tarehe 8 Agosti 2017 nchini Kenya tume ya uchaguzi nchini humo ilimtangaza Uhuru Kenyatta kuwa mshindi wa nafasi ya Urais kwa kupata kura zaidi ya milioni nane huku mpinzani wake Raila Odinga na Muungano wa NASA wakishika nafasi ya pili kwa kupata kura milioni sita.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527