MTOTO AFARIKI KWA KULIWA NA FISI KISHAPU - SHINYANGA

Fisi akila nyama,siyo ya mwili wa mtoto katika habari
Diwani wa kata ya Lagana Boniface Butondo (mwenye shati la Kitenge) na wananchi wakiwa karibu na kaburi la mtoto aliyefariki kwa kuliwa na fisi)

****
Mtoto aliyejulikana kwa jina la Katambi Masunga mwenye umri wa miaka mitano amefariki dunia baada ya kuliwa na fisi katika Kitongoji cha Mwabuli kijiji Mwamadulu kata ya Lagana wilaya ya Kishapu mkoani Shinyanga.


Tukio hilo la kusikitisha limetokea usiku wa Agosti 8,2017 kuamkia Agosti 9,2017 baada ya fisi kuvamia katika familia aliyokuwa anaishi motto huyo.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo,mtoto huyo mwenye ulemavu wa viungo akiwa na mtoto mwenzake wakicheza nyumbani kwao majira ya saa moja na nusu usiku siku hiyo,ghafla alitokea mnyama aina ya fisi.

“Baada ya kutokea fisi huyo watoto walianza kupiga kelele,huku mtoto mmoja akifanikiwa kukimbia,lakini mtoto huyo mwenye ulemavu wa viungo hakuweza kukimbia ndipo akanyakuliwa na fisi huyo”,mashuhuda wameiambia Malunde1 blog.

Baada ya fisi huyo kumnyakua mtoto huyo,alikimbia naye vichakani,kutokana na mayowe ya watoto, ndipo ndugu pamoja na majirani walipoanza kumtafuta fisi huyo.

Akizungumza na Malunde1 blog,Diwani wa kata ya Lagana,Boniphace Butondo ambaye pia ni mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kishapu alisema baada ya takribani dakika 30 ndipo wananchi wakafanikiwa kumpata fisi huyo ambaye tayari alikuwa amekula miguu na tumbo la mtoto huyo.

“Baada ya wananchi kufika katika kichaka fisi akaruka na kuanza kukimbia,waliposogea ndipo wakakuta kipande cha mwili wa mtoto kilichobakia na kukibeba”,alisema Butondo. 

“Kwa kweli hili tukio limetuhuzunisha sana,kumekuwepo na fisi wa ajabu sana eneo hili,fisi wamezaliana sana hali inayotishia amani na kuleta hofu kwa wananchi,tatizo la njaa pia linachangia hata wanyama wamekosa chakula,wamekuwa wakila hata mazao”,aliongeza Butondo. 

“Julai 28,2017 katika kikao cha baraza la madiwani moja ya ajenda ilikuwa ni kuhusu tishio la fisi katika kata tano za Itilima,Lagana,Ngofila,Uchunga na Mwamashele,tuliomba halmashauri iandae fedha maalum kwa ajili ya kuangamiza fisi hawa,utekelezaji wa kuwaangamiza fisi utaanza hivi karibuni”,alieleza Butondo.

Kata ya Lagana imekuwa ikikumbwa na matukio ya wananchi kuvamiwa na fisi ambapo hivi karibuni mzee mmoja alinusurika kufa baada ya kushambuliwa na fisi akiokoa mbuzi wake huku kukirporiwa tukio la mwanafunzi wa darasa la nne kufariki kwa kuliwa na fisi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527