MAHAKAMA YAWAACHIA HURU WAFUASI WA CUF...VURUGU YATOKEA

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imewaachia huru wafuasi 22 wa Chama cha CUF waliokuwa wakikabiliwa na mashtaka manne, likiwemo la kukutwa na mabomu ya machozi 10, ambayo yanatumiwa na Jeshi la Polisi.


Hakimu Mkazi Mwandamizi, Godfrey Mwambapa leo Jumanne, Agosti 15 amewaachia huru wafuasi hao chini ya kifungu cha 225 c ha mwenendo wa mashauri ya Jinai (CPA).


Kesi hiyo ilikuwa katika hatua ya washtakiwa hao kusomewa maelezo ya awali (PH) na leo washtakiwa hao walipaswa kusomewa, lakini Wakili wa Serikali, Nassoro Katuga amedai kuwa walikuwa bado hawajayaandaa na akaomba iahirishwe.


Hata hivyo, wakili wa washtakiwa hao, Hashimu Mziray hakuwa na pingamizi lakini Hakimu Mwambapa kutokana na kesi hiyo kuahirishwa mara kwa mara takribani mara sita aliifuta kesi hiyo na kuwaachia huru washtakiwa.


Baada ya washtakiwa hao kuachiwa huru askari polisi walianza kuwakamata kitendo ambacho kilizua purukushani kwa sababu washtakiwa hao walikuwa wakijikwamua mikononi mwa askari hao na kukimbia.


Hata hivyo, wengi wao walifanikiwa kukimbia na baadhi yao walikamatwa na kuwekwa chini ya ulinzi wa askari hao.


Pia, washitakiwa hao wanaodaiwa kutenda makosa hayo kati ya Zanzibar na Dar es Salaam wanatuhumiwa kuwa wanachama wa kikundi cha ‘Blue Guard’, kinachojitwika mamlaka ya polisi.


Washitakiwa hao waliokuwa wakikabiliwa na kesi hiyo ni Hamis Omary Hamis, Said Mohamed Zaharani, Hamid Nassoro au Hemed, Nassoro Humudi Ally, Othuman Humud au Abdallah, Swalehe Ally Swalehe na Hamis Hamis Haji.


Wengine ni Majid Juma, Mohamed Khamis Ally, Ramadhan Juma, Juma Hamad Seif, Masoud Asa Fumu, Jecha Faki Juma, Mbaruku Bakari, Muhsin Ally Juma, Juma Omary Hamis na Haji Rashid Juma.


Pia, wamo Ally Nassoro au Haji, Ally Juma Salum, Juma Haji au Mmanga, Mohamed Amir Mohamed na Mohamed Zuberi.


Kwa pamoja walikuwa wakidaiwa kuwa Septemba 20 na 25, mwaka 2016, katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar na Dar es Salaam na wenzao, ambao hawapo mahakamani, walikula njama ya kutenda kosa kwa kuunda kikosi cha brigadi, ambacho kinafanya kazi kama polisi kinyume cha sheria.


Washtakiwa hao pia wanadaiwa katika tarehe hizo na maeneo hayo, wakiwa wanachama wa kikundi cha ‘Blue Guard’, kwa madhumuni ya kujiingiza katika ajira, walikuwa wakifanya majukumu ya polisi.


Wanadaiwa kuwa Septemba 25, mwaka2016, maeneo ya Mwananyamala ‘A’, wilayani Kinondoni, Dar es Salaam, walikutwa wakimiliki visu vitano na mabomu 10 ya machozi.


Pia, wanadaiwa kuwa siku hiyo walikutwa wakimiliki mabomu hayo 10 ya machozi kinyume cha sheria, kwa kuwa kimsingi humilikiwa na Jeshi la Polisi.Walikana mashtaka hayo na walikuwa wapo nje baada ya kukamilisha masharti ya dhamana waliyopewa.


Washtakiwa hao wanatetewa na wakili Hashimu Mziray ambaye alilaani kitendo cha askari hao wa polisi kuwakamata wateja wake bila ya kufuata utaratibu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527