MKE ASHIRIKI NA MWANAE KUMUUA MUME WAKE KISA KAZIDI KWA ULEVI HUKO TABORA


Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora linawashikilia watu watatu akiwemo Tatu Said (30), Katambi Mahona (13) na Mwanza Mburuka (31) kwa tuhuma za mauaji ya Mahona Pondamali (50) mkazi wa Wilaya ya Sikonge yaliyofanyika mwezi Aprili mwaka huu.


Wakati Tatu ni mke wa marehemu, Katambi ni mtoto wa marehemu na Mburuka ni mlinzi wa jamii anayedaiwa kukodiwa na wanafamilia hao kwa malipo ya ng’ombe mmoja ili ampige marehemu kwa lengo la kumrekebisha tabia kwa sababu alikuwa mlevi wa kupindukia.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Wilbroad Mtafungwa amesema “inadaiwa wanafamilia hiyo waliandaa mpango wa kumkodi mtu wa kumpiga kwa ajili ya kumrekebisha tabia hali iliyosababisha mauti yake.” 

Alisema Aprili 4 mwaka huu, mke wa marehemu Pondamali alitoa taarifa Polisi za kupotea kwa mume wake katika mazingira ya kutatanisha na ndipo Jeshi la Polisi lilipoamua kuanza uchunguzi wa tukio hilo na kufanikiwa kubaini kuwa mtu huyo hakupotea bali aliuawa.

RPC Mtafungwa amesema kuwa uchunguzi wa awali unaonyesha kuwa marehemu alikuwa na tabia ya ulevi na baada ya kulewa alikuwa akimpiga mke wake na watoto.

Amesema kuwa baada ya wahusika kubaini kuwa amekufa ndipo walipoamua kwenda kumtupa katika shimo la wachanaji mbao.

“Polisi kwa kushirikiana na wananchi waligundua kuwa kuna mwili katika shimo la wachana mbao na kuamua kulifukua ndipo ndugu wa marehemu waliposema kuwa ni ndugu yao aliyedaiwa kupotea,” amesema.

Kamanda Mtafungwa watuhumiwa hao wanatarajiwa kufikishwa mahakamani mara baada ya upelelezi kukamilika

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527